Madiwani wilaya ya Kaskazini 'A' Unguja wafanya ziara shamba la miti Sao Hill

 

Baraza la Madiwani kutoka Wilaya ya Kaskazini A' Unguja wametembelea TFS- Shamba la Miti Sao hill leo tarehe 25 Septemba 2024 kwa lengo la kujifunza namna ambavyo shughuli za utunzaji na uhifadhi wa mazingira zinavyofanywa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania.

Akizungumza katika ziara hiyo Mstahiki Meya wa Manispaa ya Wilaya ya Kaskazini A' Unguja Bw. Machano Fadhili Machano (BABLA) amesema kuwa lengo kuu la ziara hiyo ni kujifunza namna ya ukusanyaji wa mapato, kwani asilimia kubwa ya mapato katika Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi inatokana na mazao ya misitu ikichagizwa na uwepo wa Shamba la serikali la miti ya kupandwa la Sao hill.

Aidha ameongeza ziara hiyo wanatarajia kujifunza juu ya suala zima la utunzaji wa mazingira kupitia shughuli za uhifadhi kwani TFS kupitia Shamba la miti Saohill limekuwa na utaratibu wa kushirikisha wananchi katika jukumu la uhifadhi wa misitu na hivyo  itawasaidia kufanya ushirikishaji kwa wananchi ili kuhakikisha misitu na mazingira inatunzwa.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi Mhe. Festo Elia Mgina amesema kuwa ziara hiyo ni matokeo ya uhusiano mzuri baina ya Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na Wilaya ya Kaskazini A' Unguja hivyo imelenga katika kujifunza namna Wilaya ya Mufindi imekuwa ikifanikiwa katika ukusanyaji wa mapato ya Halmashauri kupitia mazao ya misitu.

"Tumewaleta wageni wetu wajifunze katika Shamba la TFS- Sao hill ili waone ni jinsi gani limekuwa likichangia mapato makubwa katika Halmashauri zetu lakini pia jinsi linavyochangia katika huduma mbalimbali za jamii katika wilaya yetu ikiwemo ujenzi wa mabweni, madawati, zahanati, miondombinu ya barabara na elimu ya uhifadhi wa mazingira kwa kupanda miti," amesema M/kiti Mgina.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Kaskazini A' na Madiwani wote Afisa Utawala wa Baraza la Manispaa ya Kaskazini A' Husna Khamis Mohammed,  amesema kuwa ziara hiyo ina tija kubwa sana kwa madiwani wote kwani itawasaidia kubuni vyanzo vipya vya mapato na namna bora ya utunzaji wa mazingira ili kusaidia maendeleo ya wananchi wao kama ilivyo Mufindi.

Kwa upande wake Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Saohill PCO. Tebby Yoramu wakati akiwakaribisha wagaeni hao ameongeza kuwa ni faraja kubwa kwa shamba na TFS kwa ujumla, kwani unasaidia katika kuimarisha ushirikiano katika shughuli za uhifadhi pamoja na kuongeza mnyororo wa thamani unaotokana na uzalishaji wa mazao ya misitu kwani Zanzibar ni miongoni mwa wanufaika wakubwa wa mazao ya misitu yatokayo Wilayani Mufundi hususani mbao kutoka Shamba la miti Sao hill.

Katika Ziara hiyo Madiwani hao waliweza kutembelea na kuona jinsi shughuli za uvunaji wa utomvu katika miti ya misindano zinavyofanywa na kuongeza pato, pamoja na kiwanda cha kuzalisha malighafi ya nguzo za umeme cha Mufindi Woods and Poles Co. Ltd wakiwa wameambatana na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Kaskazini A' Unguja Ndg. Ali Khamis Makame pamoja na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Mufindi Ndg. George Kavenuke na Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi.

Chapisha Maoni

0 Maoni