Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Wakala wa Huduma za
MisituTanzania (TFS) itakuwa mwenyeji wa Waziri wa Utalii na Mazingira wa
Jamhuri ya Kongo na Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Tabianchi ya Bonde la Kongo
(CBCC), Mhe. Arlette Soudan – Nonault kuanzia tarehe 9 hadi 12 Septemba
2024.
Ziara hii inatoa fursa muhimu ya kukuza ushirikiano na
kuongeza uelewa kuhusu changamoto za mabadiliko ya tabianchi na uhifadhi wa
rasilimali za maliasili katika bonde la Kongo.
Akizungumza leo Septemba 9, 2024 jijini Dodoma, Kamishna wa
Uhifadhi, Prof. Dos Santos Silayo amesema Kamisheni ya Tabianchi ya Bonde la
Kongo, iliyoanzishwa Novemba, 2016 wakati wa mkutano wa COP 22 uliofanyika
Morocco, ikijumuisha nchi 17, ikiwemo Tanzania.
Anaongeza kuwa lengo kuu la Kamisheni hiyo ni kuimarisha
uwezo wa nchi wanachama katika kulinda na kuhifadhi misitu na mito ya Kongo,
ambayo ina umuhimu mkubwa katika kudhibiti hali ya hewa duniani na kukuza
maendeleo endelevu ya jamii.
Prof. Silayo anasema katika ziara hiyo Waziri na Katibu
Mtendaji wa CBCC ameongozana na wajumbe nane ambapo watafanya mkutano na Waziri
wa Maliasili na Utalii, Mhe. Pindi Chana pamoja na mazungumzo na mawaziri wa
sekta nyingine kama vile Mazingira, Mambo ya Nje, Fedha, Uchumi, na Mipango.
Aliwataja wajumbe hao kuwa ni Bi. Florantine Mapeine
Onotiang, Mkurugenzi Mkuu wa Bonde la Kongo; Bi. Yao Yao Née Aissatou Cisse,
Mshauri wa Kimataifa; Bw. Pascual Nguema Nkongo Andeme, Kiongozi wa Kazi katika
Ofisi ya Rais wa Benki ya Maendeleo ya Nchi za Kati za Afrika (BDEAC); Bw. Guy
Lié Djombe, Kiongozi wa BDEAC; Bw. Osty Destin Nzonza, Mpigapicha; Bi. Lee
Danielle Abiome; na Bw. Kessali Lekouledzela, Msaidizi wa Waziri.
“Ziara hii ina umuhimu mkubwa kwa Tanzania, ambayo kama mwanachama wa CBCC, inafaidika na utaratibu wa pamoja wa usimamizi wa rasilimali za maliasili, rasilimali fedha, na kuimarisha mifumo ikolojia ya eneo letu.
“Ujumbe huu utasaidia kuimarisha sauti ya Tanzania katika
majadiliano ya kimataifa kuhusu usimamizi wa maliasili na mabadiliko ya
tabianchi, huku ikichangia uzoefu wake na kupokea maarifa mapya kutoka kwa nchi
nyingine wanachama,” anasema.
Kamisheni ya Tabianchi ya Bonde la Kongo inajumuisha nchi 17, ambazo ni Angola, Burundi, Cameroon, Jamhuri ya Kati ya Afrika, Chad, Jamhuri ya Kongo, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Guinea Ikweta, Ufalme wa Morocco, Gabon, Kenya, Rwanda, Sao Tome na Principe, Sudan Kusini, Tanzania, Uganda, na Zambia.
0 Maoni