EU kuimarisha ushirikiano wa Uchumi wa Bluu na Tanzania

 

Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Masuala ya Bahari na Uvuvi ya Tume ya Umoja wa Ulaya, Bi. Charlina Vitcheva, anatarajiwa kutembelea Tanzania kuanzia Septemba 9 hadi 11, 2024.

Ziara yake inalenga kushiriki katika Mkutano wa nane wa Mawaziri Wanaohusika na Masuala ya Bahari, Maji ya Ndani, na Uvuvi kutoka mataifa wanachama wa Umoja wa Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS), ambao utafanyika tarehe 11 Septemba katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere. Mkutano huo unatarajiwa kuhudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Tanzania, Mh. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Ziara hii inaakisi dhamira ya Umoja wa Ulaya (EU) katika kuimarisha ushirikiano wake na Tanzania katika sekta ya uvuvi na uchumi wa bluu. Hii ni ziara ya pili ya Vitcheva, ya kwanza ikiwa Novemba mwaka jana amabapo, pamoja na shuguli nyengine, alikutana na kufanya mazungumzo Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Mwinyi.

Kabla ya kuhudhuria mkutano wa mawaziri wa OACPS, Bi. Vitcheva atatembelea Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) iliyoko Kunduchi. Wakati wa ziara hiyo, ataangalia miundombinu ya utafiti ya taasisi hiyo na kujifunza kuhusu jitihada za TAFIRI katika uhifadhi wa mfumo wa ikolojia wa baharini. Aidha, atatembelea maonyesho yatakayobainisha shughuli za uhifadhi za taasisi hiyo, ikiwa ni pamoja na maonyesho ya mbinu za kukusanya data na utafiti mwingine wa baharini. Pia atahudhuria maonyesho ya kitengo Uhifadhi wa Bahari na Maeneo Tengefu, ili kujifunza kuhusu kazi yao ya usimamizi wa bahari na juhudi za kusaidia ustawi wa jamii zinazoishi ndani ya hifadhi za bahari.

Bi. Vitcheva pia atakutana na kampuni kadhaa changa za Kitanzania zilizochaguliwa kupitia mpango wa Blue Invest Africa. Wawekezaji hawa wanabuni suluhisho za kusaidia maendeleo endelevu kupitia ya uchumi wa bluu.

Sehemu ya ratiba yake pia itajumuisha mkutano wa ana kwa ana na Mh. Abdallah Ulega, Waziri wa Mifugo na Uvuvi wa Tanzania.

Ziara ya Bi. Vitcheva inaonyesha dhamira ya EU ya kuendeleza uchumi wa bluu na usimamizi endelevu wa uvuvi nchini Tanzania. Msaada wa EU nchini Tanzania unatekelezwa kupitia programu yake kuu ya TZS bilioni 332.5 (EUR milioni 110) ya Uchumi wa Bluu kwa Ajira na Mabadiliko ya Tabianchi.

Programu hii inalenga kujenga Uchumi wa Bluu unaohimili mabadiliko ya tabianchi katika miji ya pwani ya Tanzania, Zanzibar, na Ukanda wa Kiuchumi wa Bahari ya Hindi. Programu hii inadhamiria kujenga ulinzi wa mifumo ya ikolojia ya pwani, kukuza biashara endelevu zenye ajira nyingi, na kuhimiza ukuaji wa muda mrefu kupitia mageuzi ya sera na utawala wa mabadiliko.

Chapisha Maoni

0 Maoni