Wananchi washauri mradi wa REGROW uwe wa nchi nzima

 

Wizara ya Maliasili na Utalii imeendelea kuhakikisha watanzania wanapata Taarifa na kuibua fursa mbalimbali kupitia Idara na Taasisi zake maonesho ya Wakulima Wavuvi na Wafugaji "Nanenane" pamoja na kuwajengea uwelewa wananchi juu ya Utekelezaji wa Mradi wa Kuboresha Usimamizi wa Maliasili na Kukuza Utalii Kusini mwa Tanzania (REGROW).

Akiongelea ushiriki wa  mradi wa REGROW katika maonesho hayo makubwa yanayofanyika kitaifa Jijini Dodoma, Afisa Ufuatiliaji na  Tathmini wa Mradi Bw. Michael Kalaghe, amesema lengo ni kutoa elimu kwa umma juu ya utekelezaji wa mradi na kuanika fursa na manufaa yaliyopo kwa watanzania kupitia REGROW.

Bw. Kalaghe ameongeza kuwa ushiriki wa mradi huo Nanenane licha ya kutoa elimu kwa umma, pia ni sehemu muhimu ya kupokea maoni kutoka kwa watu na wadau mbalimbali juu ya utekelezaji  wa mradi.

Aidha, Mzee Joshua Chavala ameipongeza Serikali kwa kazi kubwa inayofanya katika kuinua utalii Kusini kupitia Mradi REGROW kwani licha ya maelezo aliyopata kupitia Maonesho ya Nanenane, ameshuhudia kupitia vyombo vya habari namna wananchi wanavyonufaika kupitia Benki za Kijamii "COCOBA'.

Naye Bi. Neema Adrian Makazi wa Babati, licha ya kuipongeza Serikali kwa juhudi kubwa za kuwainua wananchi kiuchumi kupitia Mradi wa REGROW ameishauri kuupeleka Mradi huo utekelezwe kote nchini ili wananchi wafaidike na fedha za Miradi kwa jamii kama wanavyonufaika sasa na mradi huo wananchi waishio Kusini mwa Tanzania.

Mradi wa REGROW unaotekelezwa Kusini mwa Tanzania umelenga kuimarisha Usimamizi wa Maliasili, Kuwainua wananchi kiuchumi pamoja na kuchechemua utalii kwenye vivutio vilivyopo Kusini mwa Tanzania.

Na. Sixmund Begashe- Dodoma

Chapisha Maoni

0 Maoni