Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Kamishna
Benedict Michael Wakulyamba, amepongeza juhudi za Wakala wa Huduma za Misitu
Tanzania (TFS) katika kuimarisha usimamizi wa hifadhi za mikoko na utalii
wilayani Tanga.
Katika ziara yake hiyo, Kamishna Wakulyamba alitembelea
ofisi ya TFS Wilaya ya Tanga na kukutana na Mhifadhi wa Wilaya pamoja na
watumishi wa wakala, na kupokea taarifa za utendaji kwa mwaka wa fedha
2024/2025 na kujionea maendeleo ya miradi ya uhifadhi na utalii.
Mhifadhi wa TFS Wilaya ya Tanga, Lawlence Brighton Kamugisha
alieleza kuwa wakala umeanzisha Kamati za Maliasili za Vijiji (VNRC) ili
kuimarisha usimamizi wa hifadhi za mikoko kwa kushirikiana na wananchi.
Aliongeza kuwa TFS imeanzisha miradi rafiki kwa mazingira,
ikiwemo uanzishwaji wa mizinga ya nyuki, kama njia ya kupunguza utegemezi wa
kifedha kwa jamii.
"Wakala umeimarisha doria za majini kwa kununua injini
mpya yenye nguvu ya HP 115 na kufanya matengenezo makubwa ya boat ya doria, ili
kuboresha ulinzi katika wilaya za Mkinga, Tanga, na Pangani," alisema
Mhifadhi huyo.
Baada ya kupokea taarifa na kujionea shughuli za uhifadhi,
Wakulyamba alikemea uvamizi wa eneo la hifadhi la Chumvini, ambapo wananchi
wameanzisha makazi na kuharibu mazingira, huku akitia wito kwa wahifadhi
kufuata taratibu, sheria, na kanuni za uhifadhi kwa weledi na kuzingatia mila
na desturi za kiaskali.
"Wahifadhi mnapaswa kufanya kazi kwa weledi, kufuata
taratibu, sheria, na kanuni za jeshi la uhifadhi. Ni muhimu kujua sheria
mbalimbali za uhifadhi, ikiwa ni pamoja na sheria za wanyapori, General Orders,
na sheria za ushahidi," alisisitiza Wakulyamba.
katika hatua nyingine Wakulyamba alikubaliana na mipango ya
kuanzisha zao jipya la utalii katika hifadhi ya mikoko, ikiwa ni pamoja na
ujenzi wa boardwalk yenye mita 150 na maboresho ya kituo cha Malikale Tongoni.
Aidha, alishukuru kwa uimarishaji wa doria za majini na
kuwataka watumishi kuongeza majengo katika Mangrove Boardwalk ili kuvutia
wageni zaidi na kuongeza mapato.
Naibu Katibu mkuu pia Katika ziara yake alitembelea ofis za
wilaya za TFS Pangani ambapo alipongeza
jitihada za jitihada za kiuhifadhi zinazofanywa na TFS Katika uhifadhi na
usimamizi wa uvunaji na kuvuka lengo la MAKUSANYO ya Fedha za serikali, pia
alisisitiza uimarishaji wa doria kudhibiti utoroshaji wa mazao ya misitu Kwa
njia ya bandari zisizo rasmi.
Katika ziara hiyo Naibu Katibu mkuu aliambatana na Maafisa waandamizi toka makao makuu TFS na Kanda.
0 Maoni