Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma
na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu amesema Serikali imepanga kutangaza jumla ya ajira
mpya 37, 616 huku ajira za kada ya Ualimu, Afya na kada nyinginezo ikiwemo kada ya
uhasibu na ugavi zikiwa tayari
zinaendelea kutangazwa lengo likiwa ni kupunguza tatizo la upungufu wa
watumishi nchini.
Mhe. Sangu ameyasema hayo leo kwa nyakati tofauti wakati
akizungumza katika mikutano ya hadhara iliyofanyika katika vijiji vya Kitete,
Laela, Kamsamba na Kavifuti vilivyopo katika
Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga, mkoani Rukwa, ikiwa ni ziara yake
ya kwanza tangu alipouteliwa
kushika wadhifa huo.
Akizungumzia nafasi za ajira ya ualimu ambazo tayari
zimeshatangazwa na Sekretarieti ya Ajira kwenye ngazi ya mikoa kulingana na
mahitaji ya mkoa husika, Mhe. Sangu amesema utaratibu wa kuwapata walimu kwa
mwaka huu umeanza kuwa wa tofauti ukilinganisha na miaka ya nyuma.
Amefafanua kuwa usaili huo umeanza kufanyika kwa kada ya
ualimu kwa sababu nafasi za ajira za
ualimu ni chache ukilinganisha na idadi
ya walimu wa shule ya msingi na sekondari waliohitimu vyuo mbalimbali hapa
nchini ambapo zaidi ya walimu100,000 wapo mtaani wakiwa hawana ajira.
Amesema Serikali imekuja na uamuzi huo ili kuchagiza dhana
ya ushindani kwa lengo la kuhakikisha kila mwenye sifa stahiki anapata ajira
katika mazingira aliyopo pasipo kulazimika kusafiri kwenda Dodoma au Dar es
Salaam kwa ajili ya kufanya usaili.
Kufuatia hatua hiyo, Mhe. Sangu ametoa wito kwa vijana waliohitimu
vyuo mbalimbali hapa nchini kuchangamkia nafasi hizo za ajira huku akiwataka
wajiandae ipasavyo kwa ajili ya usaili huo, ikiwa ni mara ya kwanza kwa kada
hiyo ya ualimu kufanya usaili
Ametumia fursa hiyo kuwatoa wasiwasi wote walioomba nafasi
hizo za ualimu huku akiwahakikishia kuwa Ofisi yake yenye dhamana ya kusimamia
masuala ya ajira nchini imejizatiti kuhakikisha mchakato huo wa kuwapata walimu
wenye sifa stahiki utakuwa wa huru na haki.
“Katika kumsaidia Waziri wangu Mhe, George Simbachawene tutahakikisha sera ya ajira nchini inayosisitiza haki ya kupata ajira bila kujali hali ya kiuchumi, rangi, kabila na dini inazingatiwa kikamilifu,” Mhe. Sangu.
Na. Lusungu Helela- Rukwa
0 Maoni