Muhimbili Mloganzila yageuka lulu baada ya kuimarika kwa huduma

 

Kutokana na kuimarika kwa huduma bora za kibingwa na ubingwa bobezi Hospitali ya Taifa Muhimbili -Mloganzila imeendelea kuaminika na kuwa kivutio cha matibabu nje na ndani ya nchi, hivyo kupelekea ongezeko la wagonjwa wa nje (OPD) kutoka 600 kwa siku mwaka 2022 hadi kufikia wagonjwa 1117 mwaka 2024.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Mkurugenzi Mtendaji MNH-Mloganzila, Dkt. Julieth Magandi wakati akielezea mwenendo wa utoaji wa huduma katika hospitali hiyo na kuongeza kuwa imani kwa wananchi kuhusu huduma zinazotolewa Muhimbili Mloganzila imeongezeka sana ukilinganisha na miaka miwili iliyopita.

Dkt. Magandi ameongeza kuwa sambamba na kuongezeka kwa wagonjwa wa nje, idadi ya wagonjwa wanaolazwa imeongezeka pia kwa asilimia 70 hadi 80 kufikia 2024 ukilinganisha na asilimia 40 kwa mwaka 2022.

“Tumeendelea kuimarisha usimamizi wa huduma ikiwa ni pamoja na kusikiliza maoni, ushauri, malalamiko ya wateja na kuyatafutia majawabu na kuhakikisha kuwa wananchi wanapata mrejesho kwa wakati kitu ambacho kwa namna moja ama nyingine kimeendelea kuimarisha uhusiano wetu na wale tunaowahudumia,” ameongeza Dkt. Magandi.

Dkt. Magandi amebainisha kuwa ongezeko hilo limechagizwa pia na kuongezwa kwa wigo wa kliniki za kuona wagonjwa wa nje ikiwemo kliniki za mifupa, fiziotherapia pamoja na watoto ambazo pia zinafanyika siku za jumamosi uanzishwa huduma za kiliniki za jioni.

Kwa mujibu wa Dkt. Magandi hospitali hiyo itaendelea kutoa huduma bora na zilizotukuka kwa wananchi na kufanya kila Mtanzania kutamani kufanyiwa uchunguzi na matibabu Muhimbili Mloganzila na hivyo kufikia lengo walilojiwekea la kuona wagonjwa wa nje 1,500 kwa siku siku za usoni.

Chapisha Maoni

0 Maoni