BENKI ya Dunia imeipongeza Tanzania kwa hatua kubwa
iliyopiga katika kutekeleza mradi wa kimkakati wa Reli ya Kisasa-SGR kwa kuwa
ni miongoni mwa miradi itakayochochea ukuaji wa uchumi wa nchi pamoja na
kuboresha huduma ya usafiri na usafirishaji kwa wananchi.
Pongezi hizo zimetolewa mjini Abuja nchini Nigeria na Makamu
wa Rais wa Benki ya Dunia anayesimamia nchi za Ukanda wa Mashariki na Kusini
mwa Afrika, Bi. Victoria Kwakwa, alipokutana na ujumbe wa Tanzania ukiongozwa
na Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Kando ya Mikutano wa
Mawaziri wa Fedha na Magavana wa Benki Kuu za Nchi za Afrika, ambazo ni
wanachama wa Benki ya Dunia na Shiruka la Fedha la Kimataifa-IMF.
Dkt. Victoria Kwakwa, amesema kuwa si rahisi kwa nchi nyingi
za Afrika kujenga mradi mkubwa wa reli kama ilivyofanya Tanzania kwa kuwa ina
gharama kubwa lakini kukamilika kwake kutachochea biashara katika eneo la
Maziwa Makuu huku akimmwagia sifa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuzindua rasmi safari za treni hiyo kutoka
Dar es Salaam kwenda Dodoma.
Kwa Upande wao, Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck
Nchemba (Mb) na Katibu Mkuu na Mlipaji Mkuu wa Serikali Dkt. Natu El-maamry
Mwamba, walipokea pongezi hizo kwa niaba ya Serikali na kueleza kuwa lengo la
mradi huo ni kuunganisha baadhi ya nchi za Ukanda wa Afrika Mashariki ili
kufungua milango ya biashara.
Dkt. Nchemba alitumia mazungumzo hayo kuzitaka Taasisi za
Fedha za Kimataifa ikiwemo Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa IMF,
kuangalia uwezekano wa kuweka riba nafuu kwenye mikopo inayotolewa kupitia
madirisha ya ujenzi wa miundombinu ili nchi za Afrika ziweze kuboresha
miundombinu ya usafiri na usafirishaji hatua itakayochangia kukamilisha miradi
husika kwa wakati.
Benki ya Dunia ni mdau mkubwa wa maendeleo ya Tanzania ambapo imewekeza kiasi kikubwa cha fedha katika miradi mbalimbali ya kimkakati ya maendeleo pamoja na kuchangia Bajeti Kuu ya Serikali.
Na. Benny Mwaipaja- BOT
0 Maoni