Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe Angelah Kairuki
amempongeza Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. Samia Suluhu
Hassan kwa kutoa magari 22 kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS)
yatumike kwenye usimamizi wa raslimali
za misitu nchini ili kuwakomboa wanawake waachane na nishati chafu za kuni na
mkaa ambazo zimekuwa zikiwaletea changamoto nyingi na kinara wa matumizi ya nishati safi Afrika.
Mhe. Kairuki ametoa kauli hiyo leo Mei 24 wakati alipokuwa
akikabidhi kwa menejimenti ya TFS magari
22 yaliyonunuliwa wa Serikali
yatakayotumika katika usimamizi wa misitu katika kanda zote saba hapa nchini yenye thamani ya shilingi bilioni
4.3 ikiwa ni Toyota Prado VXL, 7 zilizogharimu shilingi
bilioni 2.2 kwa ajili ya Wakuu wa Kanda hizo na Toyota LandCruiser
Hardtop, 12 zilizogharimu shilingi bilioni 2.1 zitakazotumika na Maafisa kwenye
maeneo yote ya kanda. Hiyo ikiwa ni awamu ya kwanza ambapo awamu ya pili
serikali itatoa magari tisa aina ya Toyota LandCruiser Hardtop.
Amefafanua kuwa ukiachana na uharibifu wa mazingira unaotokana na matumizi ya nishati chafu ya kupikia kama
kuni na mkaa tumeendelea kushuhudia majanga mengi
yakitokea katika mazingira na
afya ya binadamu ambapo mwanamke amekuwa mhanga mkubwa wa
masuala haya kwa sababu kwa kiasi
kikubwa ndiyo watafutaji na
watumiaji wa nishati chafu za mkaa na kuni
zinazotokana na ukataji wa misitu hivyo magari hayo yametasaidia kwenye
doria na usimamizi wa raslimali za misitu.
Ameongeza kuwa kutokana na umuhimu huo, Mei nane mwaka huu, Mhe.
Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alizindua rasmi mkakati wa miaka 10 wa Taifa wa
Matumizi ya Nishati Safi ya kupikia kutoka mwaka 2024 hadi 2034
unaohusisha pia masuala mbalimbali
ikiwemo kuongeza uelewa wa wananchi
kutumia Nishati Safi ambao umelenga
kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 zaidi ya asilimia 80 ya wanawake wote
nchini waweze kutumia nishati safi.
Ametaka magari hayo
yawe chachu ya kuwaongezea ari ya
kufanya kazi kwa ubunifu, bidii na maarifa na
kufika maeneo ya mbali zaidi huku
wakiyatumia kwa uangalifu ili kuleta tija iliyo kusudiwa ya kutoa elimu ya uhifadhi wa misitu, kufanya
doria za kimkakati na kufanya usimamizi wa raslimali za misitu kwa ujumla.
Aidha, ameitaka TFS kufikiria kuanzisha mazao mapya ya
utalii wa ikolojia, miundombinu ya malazi kwa wageni na kuchangamkia biashara ya Cabon huku wakiendelea kuandika maandiko
ya miradi ili kuliingizia fedha taifa.
Amesema ni muhimu kuthamini na kutekeleza kwa vitendo maono
ya Mhe. Rais ya kutangaza Tanzania kama alivyofanya kwenye Filamu ya The Royal
Tour na hivi Karibuni Filamu ya Amaizing Tanzania iliyozinduliwa Beijing China
Mei 15 mwaka huu.
Awali, akimkaribisha Mhe.Waziri Naibu Katibu Mkuu wa Wizara
ya Maliasili na Utalii, CP Benedict Wakulyamba ambaye ndiye Msimamizi Mkuu wa
Jeshi la Uhifadhi amemshukuru Mhe. Rais kwa kuendelea kuijengea uwezo TFS kwa
kutoa fedha nyingi kununua vitendea kazi vya kisasa vya kufanyia kazi ya
uhifadhi.
“Naomba niwe muwazi, katika kipindi chote cha utumishi wangu, katika kipindi hiki kifupi cha Mhe. Rais Samia amefanya maboresho ya kisasa kwa kusaidia kuleta vifaa vya kidigitali na magari, ninamshukuru na kumpongeza sana Mhe. Rais,” ameongeza CP Wakulyamba.
Kwa upande wake, Kamishna wa Uhifadhi wa TFS, Prof. Dosantos
Silayo amemhakikishia Waziri Kairuki kuwa Menejimenti yake imejipanga vizuri
ili kuhakikisha kuwa magari hayo yatakwenda kuongeza ufanisi mkubwa na
kuliingizia taifa mapato zaidi.
Amesisitiza kuwa kwa sasa TFS inatumia teknolojia ya kisasa
ambayo itasaidia kuboresha usimamizi
wa maeneo makubwa ya misitu na
nyuki hapa nchini.
Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Bodi ya TFS, Dkt. Siima Makengeza, Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki wa Wizara ya Maliasili Deusdedith Bwoyo, Wasimamizi wa kanda zote saba za TFS na maafisa mbalimbali wa Wizara.
Na. John Mapepele
0 Maoni