Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda
amesema Serikali imeanzisha udhamini (Scholarship) maalum kwa wanafunzi
wanaofaulu masomo ya Sayansi ambapo watasomeshwa na Serikali kwa asilimia 100
kwa gharama zote zikiwemo za kujikimu, chakula, mabweni na vifaa vya elimu hadi
mwanafunzi atakapomaliza masomo yake.
Prof. Mkenda amesema hayo jijini Tanga katika maadhimisho ya
Wiki ya Kitaifa ya ya Elimu, Ujuzi na
Ubunifu yanayozikutanisha taasisi, mashirika, wadau wa maendeleo, asasi,
watunga sera, wabunifu/wagunduzi na
wadau wengine kutoka ndani na nje ya nchi, kwa ajili ya mijadala na
kubadilishana uzoefu juu ya masuala ya elimu, ujuzi na ubunifu.
“Kama wewe ni mwanafunzi unasoma masomo ya sayansi ukafaulu
kidato cha sita kati ya wanafunzi bora 640 hadi 700 hapa nchini ukaamua kusoma
vyuo vya ndani Tanzania kwenye nyanja za Sayansi, Uhandisi, Elimu Tiba, TEHAMA
au Hisabati, wanafunzi hao watasomeshwa kwa asilimia 100 na Serikali, sio
mikopo Serikali itakulipia gharama zote na hii inaitwa ‘Samia Scholarship,” amesema
Prof. Mkenda.
Ameongeza kuwa maadhimisho hayo ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yatafanyika mkoani Tanga kwa miaka mitatu mfululizo ikiwa ni sehemu ya mikakati ya Serikali katika kuongeza hamasa ya kukuza elimu, ujuzi, na matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu kama nyenzo za kusaidia kutatua changamoto za kiuchumi na kijamii pamoja na kuchagiza maendeleo ya nchi kwa ujumla.
0 Maoni