Waziri wa Maliasili
na Utalii Mhe. Angellah
Kairuki ametangaza rasmi matokeo
ya sensa ya wanyamapori katika
mifumo mitatu ya ikolojia ya Nyerere-Selous-Mikumi, Saadani-Wamimbiki
na Serengeti ambayo ni miongoni mwa mifumo
11 ya ikolojia nchini.
Akitangaza matokeo hayo katika mkutano wa wadau wa uhifadhi
na utalii uliofanyika jijini Arusha, Mhe. Kairuki amesema, sensa katika
mfumo ikolojia wa Nyerere-Selous-Mikumi,
unaonesha kuimarika kwa spishi 22 za
wanyamapori wakiwemo nyati/buffaloes (59,878), tembo/elephants (20,006),
nyumbu/wildebeest 19,060, kongoni/hartebeest (18,361), swalapala/impala
(14,031), ngiri (13,806) na idadi ya Wanyama walioonekana kwa idadi ndogo ni
twiga/giraffe (1,679), Tandala mkubwa/greater kudu (1,414) na puku/sheshe
(496).
"Katika mfumo huu
kumekuwa na ongezeko la tembo
20,006 (2022) ikilinganishwa na sensa ya awali 15,501 (2018) na Viashiria vya ujangili wa tembo
au vifo vya tembo vimepungua kwa kiasi kikubwa
kutoka 16% mwaka 2018 hadi hadi 0.8% mwaka 2022," ameeleza Mhe. Kairuki.
Mhe. Kairuki ameitaka Idara ya Wanyamapori Wizara ya Maliasili na
Utalii kuchukua hatua za haraka kulinda idadi ya Sheshe/puku ambao
wanapatikana Tanzania pekee waliosalia katika maeneo yao ya asili
yakiwemo mapori ya akiba ya Kilombero na ziwa Rukwa ambao idadi yao imepungua kwa kiasi kikubwa kutoka (1,579 mwaka 2018) hadi (496 mwaka 2022).
Vilevile, uhesabuji wa Nyumbu katika mfumo ikolojia wa
Serengeti matokeo ya sensa hii yamebaini uwepo wa nyumbu wanapatao 1,597,850.
Idadi hii inaonyesha kuimarika kwa nyumbu ikilinganishwa na sensa ya hapo awali
(2015) iliyoonyesha uwepo wa nyumbu wapatao 1,326,709.
Kwa upande wa mfumo ikolojia
wa Saadani - Wami - Mbiki Matokeo ya sensa yameonesha uwepo wa wanyamapori wachache unahusishwa na hali ya upya wa hifadhi hizi
ambapo hapo awali,hifadhi ya Saadani ilikuwa pori tengefu na sehemu nyingine
ilikuwa shamba la mifugo na zoezi la kuongeza wanyamapori lilifanyika miaka ya
hivi karibuni .
Aidha , Mhe. Kairuki amesema kwa mwaka wa fedha 2024-2025 wizara imeweka mikakati ya kufanya sensa ya wanyamapori katika mifumo yote ya ikolojia kwa lengo la kuimarisha uhifadhi na kukuza kuwa na utalii endelevu ambapo ametoa rai kwa wadau kuonga mkono jitihada hizi za Serekali katika kuhifadhi utajiri wa Maliasili ya Wanyamapori .
0 Maoni