Wananchi walioathiriwa na mafuriko wilayani Rufiji wameiona thamani na umuhimu
wa uwepo wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania - TAWA baada ya
leo Aprili 16, 2024 kupokea misaada
mbalimbali kutoka kwa taasisi hiyo yenye
thamani ya shillingi millioni 20 ikiwemo tani 6.4 za unga wa sembe, Kilo 666 za
maharage na magodoro 186.
Kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA akimkabidhi
misaada hiyo Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakari Kunenge, Kamishna Msaidizi
mwandamizi Abraham Jullu amesema TAWA imeguswa na janga la mafuriko
lililowapata majirani na wadau namba moja wa uhifadhi wananchi wa Rufiji ambao
wamehusika kwa kiasi kikubwa kulinda rasilimali za Hifadhi ya Selous na hivyo
imelazimika kuwashika mkono.
Jullu amesema tangu changamoto hii ya mafuriko imejitokeza
TAWA ilifika kwa haraka na kuongeza nguvu kwa kutoa kikosi cha Askari 24 ili
kusaidia katika zoezi la uokozi ikiwa ni pamoja na kutoa elimu ya mbinu za
kujikinga na madhara yatokanayo na wanyamapori wakali na waharibifu hususani
mamba na viboko kwa jamii ambapo mpaka sasa TAWA imetoa elimu hiyo kwa wananchi
wapatao 4,225 na bado inaendelea na zoezi hilo.
Sanjari na hilo, TAWA imetoa boti moja lenye uwezo wa kubeba
jumla ya watu 15 ili kusaidia katika shughuli za uokozi zinazoendelea wilayani
humo.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakari Kunenge
amemshukuru Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kwa kupeleka misaada mbalimbali kupitia Serikali na Chama Cha
Mapinduzi tangu wilaya hiyo ipate changamoto hiyo ya mafuriko.
Pia amewashukuru
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TAWA Mej. Jen. (Mstaafu) Hamis Semfuko na
Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA Mabula Misungwi Nyanda kwa maamuzi ya haraka
waliyoyafanya kupeleka misaada hiyo kwa wananchi wa Rufiji kwa wakati.
Mkuu huyo wa Mkoa ameendelea kuishukuru TAWA kwa msaada wa
boti kwa ajili ya kufanya shughuli za
uokozi na ushiriki wao wa ujumla katika zoezi la uokozi kwa kushirikiana
na vyombo mbalimbali vya dola na kukiri kuwa wananchi wa Rufiji wanaona thamani
na umuhimu wa uwepo wa Taasisi hiyo Mkoani Pwani.
Licha ya kuishukuru TAWA, Mkuu wa wilaya ya Rufiji Meja Edward Gowele amesema TAWA imekuwa na mahusiano na mashirikiano mazuri kati yake na uongozi wa wilaya yake ndio maana imekuwa rahisi kwao kuitikia wito wa kutoa msaada kufuatia janga lililoikumba wilaya hiyo.
Na. Beatus Maganja- Rufiji
0 Maoni