Tanzania inaendelea
kujivunia kuwa na utajiri mkubwa wa Rasilimali ya Wanyamapori ambapo inashikilia nafasi ya kwanza barani Afrika kwa kuwa na idadi kubwa ya Simba, Chui na Nyati.
Haya yalibainishwa na Mkurugenzi Mkuu
wa Taasisi ya
Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) Dkt.
Eblate Ernest Mjingo
katika hafla ya uzinduzi wa matokeo ya sensa ya wanyamapori katika mifumo ikolojia mitatu ya Nyerere-Selous-Mikumi, Saadani-Wamimbiki na
Serengeti.
Dkt. Mjingo alieleza kuwa, kwa mujibu wa taarifa ya
Umoja wa Kimataifa wa Uhifadhi na
Kulinda Ualisia (IUCN) ya mwaka 2023, Tanzania inaongoza kwa kuwa na idadi
kubwa ya simba barani Afrika, ambapo ina
jumla ya simba 17,000 ikifuatiwa na
Afrika Kusini yenye simba 3,300 na
Botswana yenye Simba 3,064.
Vilevile, kwa upande
wa nyati Tanzania inashika nafasi ya
kwanza kwa kuwa na nyati 225,000, ikifuatiwa na Afrika Kusini yenye nyati 46,000 na ya tatu ni
Msumbiji yenye nyati 45,000.
Kwa upande wa chui Tanzania inaendelea kushika rekodi ya kwanza kwa kuwa na idadi ya
chui 24,000 sambamba na kushika nafasi
ya tatu kwa kuwa na tembo 60,000.
Aidha, Dkt. Mjingo amebainisha hali ya ustawi wa uhifadhi wa wanyamapori hapa nchini ni kutokana na juhudi kubwa za Serikali katika kuhifadhi ambapo imeendelea kuwezesha tafiti mbalimbali kufanyika pamoja na sensa za wanyamapori sambamba na mchango mkubwa wa usimamizi na ulinzi shirikishi wa Mamlaka za Uhifadhi za TANAPA, TAWA na Ngorongoro.
0 Maoni