Serikali imeipa umuhimu mkubwa sekta ya miundombinu hususani
kwenye ujenzi na matengenezo ya barabara za vijijini na kumfanya mwananchi
kufika kusiko fikika.
Hayo yameelezwa na Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za
Vijijini na Mijini (TARURA), Mhandisi Victor Seff wakati akielezea mafanikio ya
miaka mitatu ya Serikali ya Awamu ya Sita jijini Dar es Salaam.
Mhandisi Seff alisema kwamba yapo mengi yaliyofanyika na
Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kipindi cha miaka
mitatu hususan upande wa barabara.
Alisema barabara za vijijini ni muhimu sana kwani asilimia
65.1 ya watanzania wanaishi vijijini na
shughuli zao kubwa hutegemea kilimo
hivyo Serikali imeona umuhimu huo kwa kuongeza bajeti ya barabara na kuweza
kutengeneza barabara maeneo ya vijijini.
"Serikali inatoa umuhimu kwa barabara za vijijini
ikiwemo kuongeza bajeti mara tatu ukilinganisha na miaka ya nyuma na kufanya
maeneo mengi kufikika,” aliongeza.
Aidha, Mhandisi Seff alitaja mkakati wa TARURA ifikapo mwaka
2025/2026 ni kufikisha asilimia 85 ya barabara zilizo korofi kupitika bila
shida yoyote.
“Asilimia 69.1 ya barabara zilizobaki ni udongo na hivyo
huathiriwa na mvua zinaponyesha na kufanya maeneo mengi kutopitika ila mkakati
wetu hadi kufika mwaka 2025/2026 asilimia 85 zitakuwa zinafikika bila shida.”
Naye, Kaimu Mratibu wa
kikosi kazi kinachosimamia miradi
inayofadhiliwa na Benki ya Dunia, Mhandisi Nyariri Nanai alisema TARURA
imeshasaini mradi wa DMDP-2 na hivyo utekelezaji wake utaifanya Dar es Salaam
kuondokana na mafuriko kwani mradi utajenga Km. 90 za mifereji ya maji na awamu
hiyo ya pili itatekelezwa katika halmashauri zote tano.
Wakati huo huo Meneja wa TARURA mkoa wa Dar es Salaam,
Mhandisi Geofrey Mkinga alisema Mhe. Rais ameongeza bajeti ya ujenzi na
matengenezo ya barabara kwa mkoa wa Dar es Salaam kutoka bilioni 20 hadi
kufikisha bilioni 49 na hivyo kufanikiwa kuongeza kutengeneza sehemu kubwa ya
barabara za jiji ambazo hapo awali zilikuwa zikiwasumbua wananchi.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa mtaa wa Mtambani mkoa wa Dar es
Salaam, Bw. Abdallah Kitumbi aliishukuru
Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapelekea
miundombinu ya barabara na mifereji ya maji na kuweza kuwaondolea adha ya
mafuriko na kuahidi wataendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa
kutunza miundombinu ikiwemo kusafisha mifereji.
0 Maoni