SHIRIKA la Nyumba la Taifa (NHC) limetoa msaada wa vyakula
mbalimbali kwa Kituo cha Mafunzo ya Watoto Al Madina kilichopo Msakuzi, Mbezi
Mkoani Dar es Salaam kwa ajili ya futari kwa watoto wanaoishi katika mazingira
magumu kwenye kipindi hiki wakiwa katika funga ya mwezi mtukufu wa Ramadhan.
Akizungumza na Waandishi wa Habari Mbezi Mkoani Dar es Salaam
Afisa Uhusiano wa Shirika la Nyumba la Taifa, Yamlihery Ndullah amesema jukumu
la kutoa msaada kwa watoto hao ni jukumu la jamii nzima kwani katika watoto hao
watapatikana viongozi wa dini na Taifa hapo baadaye.
Aidha, Ndullah amesema jambo hilo ni muendelezo wa Shirika
katika kuendelea kutoa misaada kwenye sehemu mbalimbali zenye mahitaji, pia
kupitia kwa Mkurugenzi wa NHC Hamad Abdalah, wataendelea kutoa misaada hiyo ili
kuendelea kupeleka faraja na furaha kwa watu wote Nchini.
Kwa upande wake, Imamu wa Msikiti wa Al Madina Sheikh Jumaa
Salum Mhando ambaye kituo hicho kipo chini yake
amelishukuru Shirika la Nyumba la Taifa kwa msaada huo mkubwa ambao
utawasaidia watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu kuweza kufuturu na kufunga
funga zao vyema katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhan.
"Lengo ni kuwawezesha na kuwakamua katika hali ya
kimaisha kwa kuwa wanaishi kwenye mazingira magumu, hivyo tunawapongeza NHC kwa
kuleta neema hii katika mwezi maalumu kwa sababu mwezi huu ni mwezi wa kuchuma
heri nyingi, waliofanya hivi Mungu atawazidishia zaidi ya hapa na Mungu
atawajalia wepesi katika shughuli zao," amesema Sungura.
Hivyo, Imamu wa Msikiti wa Al Madina Sheikh Jumaa Salum
Mhando ametumia nafasi hiyo kuwaomba wadau mbalimbali kuwasaidia katika kutoa
sadaka ambazo zitawasaidia kuwakwamua watoto ambao wanapitia wakati mgumu, pia
kuwasaidia katika kumalizia jengo hilo la msikiti ambalo bado halijakamilika.

0 Maoni