Mkurugenzi Mkuu Taasisi ya utafiti wa wanyamapori Tanzania
(TAWIRI) Dkt. Eblate Ernest Mjingo amesema Taasisi hiyo
imeanza rasmi zoezi la kuwatoa Tembo mikanda ya visukuma mawimbi
(GPS Collars ) katika Wilaya za
Longido, Hanang, Babati, Monduli ambapo kuna shoroba za wanyamapori zilizopitiwa na mradi wa Njia ya Umeme ya Msongo wa kV 400 wa Kenya - Tanzania Power
Interconnection Project (KTPIP).
Akizungumza Wilayani
Longido, Dkt.Mjingo ameeleza kuwa
katika Mradi wa KTPIP unaokatiza maeneo
ya Shoroba za wanyamapori za Tanganyeeti
na Laasarack Wilayani Longido, Ushoroba
wa Kwakuchinja Wilayani Babati, Mswakini chini Wilayani Monduli na Pori
la akiba la Swagaswaga, TAWIRI imefanya tafiti
na kuishauri Serikali kupitia
TANESCO ili kuwa na uhifadhi endelevu
nchini.
"Ili kupata
taarifa za kisayansi ,njia mbalimbali za
kitafiti zimeendelea kutumika katika mradi huu ambapo mwaka 2019
tuliwafunga Tembo 30 GPS Collars katika shoroba hizo kwa lengo la kufuatilia kama wanyama
wataendelea kupita baada ya kutekeleza mradi. Matokeo ya awali yameonyesha wanyama wameendelea kupita hata
baada ya miundombinu kusimikwa na
ufuatiliaji unaendelea pale umeme
utakapowashwa, " amefafanua Dkt. Mjingo.
Mkuu wa Wilaya ya
Longido Mhe. Marco Ng'umbi, wakati wa
kuwatoa Tembo GPS collar Wilayani humo, amesema Serikali ya
awamu ya sita
chini ya uongozi
shupavu wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inahakikisha kunakuwa na uhifadhi
endelevu nchini, ambapo katika kuwaletea watanzania maendeleo kupitia miradi
ya kimkakati inafanya tathimini ya athari za kimazingira na kijamii ambapo
hupata ushauri sahihi wa kisayansi kupitia tafiti.
Naye, Mhandisi John Lazimah kutoka Shirika la Umeme Tanzania
(TANESCO) ambaye pia ni Mhandisi mazingira katika Mradi huu wa (KTPIP), amesema
mradi huo unaunganisha Nchi za Kenya na Tanzania unalenga kuunganisha mfumo wa umeme wa Nchi za Afrika Mashariki ( Eastern African Power
Pool) na kuziwezesha nchi hizi kuuziana
umeme, kwa Tanzania mradi unatekelezwa kutoka Singida hadi Namanga
kupitia kituo cha kupooza umeme cha Lemugur- kilichopo Kisongo Mkoani Arusha.
Aidha, Mhandisi Lazimah
amebainisha kwamba Tanzania
inaendeleaa kukua kiuchumi kupitia mradi wa KTPIP kwa kuzalisha umeme wa
ziada na kuuza kwa nchi nyingine, Pia
kuwa na umeme wa uhakika kunapokuwa
na uzalishaji mdogo wa umeme nchini kutokana na sababu zisizo
epukika, nchi inaweza kununua kutoka
nchi nyingine na kuwezesha
shughuli za kiuchumi na kijamii zinazotegemea umeme kufanyika bila kuathirika.
Kwa mujibu wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) mradi huu wa Kenya -Tanzania Power Interconnection Project unagharimu kiasi cha Dola za kimarekani 258 Milioni na unatarajiwa kukamilika mapema mwaka huu.
0 Maoni