Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI Mhe. Mohamed
Mchengerwa ameelekeza OR-TAMISEMI na TARURA, kuanzisha mchakato wa upatikanaji
wa hati fungani ya miundombinu ya Barabara (TARURA Infrastructure Bond) ambayo
itaitwa ‘SAMIA Bond’ kwa kushirikiana na taasisi za kifedha.
Mhe. Mchengerwa ameyasema hayo leo tarehe 24 Januari, 2024
kwenye kikao kazi cha Wizara yake ya Ofisi ya Rais TAMISEMI ,TARURA, Makatibu
Tawala Wasaidizi (Miundombinu), Makandarasi Wazawa,Wataalamu Washauri na
Taasisi za Kibenki kilichofanyika kwenye ukumbi wa kituo cha Mikutano cha
Kimataifa cha Mwalimu Nyerere (JNICC ) Jijini Dar es Salaam.
Waziri Mchengerwa Amesema kwamba lengo la kuanzishwa kwa
hati fungani hiyo ni kuwasaidia Makandarasi Wazawa kukabiliana na changamoto za
kifedha wanazokupambana nazo na kuwawezesha ili miradi umwanayokuwa wamepewa
iweze kukamilika kwa wakati na ufanisi.
“Matarajio yangu ni kuwa, hati fungani hii italeta mapinduzi
makubwa kwenye sekta ya miundombinu ya Barabarainayojengwa na TARURA na
itaendana na kasi ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwashirikisha na
kufanya kazi na sekta binafsi, katika kutatua na kubuni mbinu za kuchochea
gurudumu la kuwafikishia maendeleo wananchi,” amesema Mhe. Mchengerwa.
Waziri Mchengerwa amesema kwenye eneo muhimu la matengenezo
ya barabara, fedha hupatikana kutokana na makusanyo ya kila mwezi hivyo
matengenezo hutegemea kupatikana kwa fedha baada ya makusanyo, na kuongeza kuwa
hali hii wakati mwingine husababisha matengenezo kuchelewa.
“Tafiti mbalimbali za Benki ya Dunia zinaonesha kwamba kuna
madhara makubwa kiuchumi pale kazi za matengenezo ya barabara zinaposubiri au
kuahirishwa na wameonesha kwamba ukiwekeza Dola Moja ya Kimarakeni kwenye
matengenezo ya barabara zilizo katika hali nzuri sasa utaokoa Dola Nne hadi
Kumi za Kimarekani kulinganisha na iwapo matengenezo hayo yangeahirishwa.”
Hata hivyo amesema ndoto yake ni kuwatengeneza Wakandarasi
wazawa mabilionea ambao watafanya kazi bila kushikwa mkono na kuishi ndoto ya
kumsaidia Rais Dkt. Samia.
Kikao kazi hicho kwa upande wa TAMISEMI Kimehudhuriwa pia na Naibu Waziri wa OR TAMISEMI Mhe.Deo Ndejembi,Naibu katibu Mkuu OR TAMISEMI anayeshughulikia Miundombinu Maandisi Rogatus Mativila,Mtendaji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seff pamoja na wawakilishi wengine Mbalimbali wa Wizara na Kamati ya kudumu ya Bunge ya TAMISEMI.
0 Maoni