Watoto watatu waliozaliwa na changamoto ya kutokusikia, leo
kwa mara ya kwanza wameanza kusikia sauti baada ya kufanyiwa upandikizaji wa kuwekewa
vifaa vya kusaidia kusikia na kuwashiwa vifaa hivyo ikiwa ni mwezi mmoja baada
ya upasuaji huo unaofanywa na madaktari wa Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Akizungumza wakati wa kuwasha vifaa hivyo, Mkurugenzi
Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Prof. Mohamed Janabi amesema upasuaji
huu unawapa nafasi watoto hao kuweza kusikia kama watoto wengine na kuendelea
na maisha ya kawaida.
“Leo tumewasha vifaa vya kusaidia kusikia kwa watoto watatu
ambao walikuwa hawajawahi kusikia sauti tangu walipozaliwa, hivyo wataweza
kwenda kusoma shule za kawaida kwani wana akili kama watoto wengine,” amesema,
Prof. Janabi.
Prof. Janabi amewahimiza wazazi wenye watoto ambao
wamezaliwa na hawaskii kufika hospitalini mapema ili kufanyiwa uchunguzi na
kupatiwa huduma stahiki kwani hadi kufikia miaka mitano watoto wanaweza kupata
huduma hii na kuwapa fursa ya kuishi kama watoto wengine.
Akizungumza kabla ya
kuwasha vifaa hivyo, Mtaalamu wa Mashine za zinazopandikizwa kwa watoto ili
kuwasaidia kusikia Bw. Fayaz Jaffer
amesema vifaa hivyo vinahitaji uangalizi wa hali ya juu hivyo amewasisitiza
wazazi na ndugu wa watoto hao kuwaangalia watoto hao kwa karibu zaidi ili
wasiharibu vifaa hivyo.
Ameongeza kuwa gharama za kupandikiza vifaa hivyo ni kubwa
hivyo walezi wafuate maelekezo wataliyopewa na wataalam na wahakikishe
wanaendelea kuwaleta katika kliniki ili kuona maendeleo yao na kufanyiwa
matengenezi kinga ya vifaa hivyo kama inavyotakiwa.
Huduma ya
upandikizaji vifaa hivi kwa hapa Tanzania ni TZS. 45 milioni ambapo mtoto akienda
nje ya nchi ni karibu TZS. 120 milioni. Hadi sasa Hospitali ya Taifa Muhimbili
imepandikiza watoto 66 tangu kuanzishwa huduma hiyo hapa nchini mwaka 2017.
0 Maoni