Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imejipanga
kujenga madaraja 189 kwa kutumia teknolojia ya mawe katika mikoa yote ishirini
na sita nchi nzima kwa mwaka wa fedha 2023/2024.
Hayo yameelezwa na Mratibu wa madaraja hayo, Mhandisi
Pharles Ngeleja wakati Waziri wa Ujenzi Mhe. Innocent Bashungwa alipotembelea
banda la TARURA kwenye Kongamano la Kitaifa la 32 la Taasisi ya Wahandisi
Tanzania lililofanyika kwa siku mbili katika Kituo cha Kimataifa cha Mkutano
Arusha (AICC).
Mhandisi Ngeleja alisema hadi sasa wameweza kujenga madaraja
56 ya mawe ambapo utaratibu wa ujenzi wa madaraja mengine unafanyiwa kazi.
Alisema teknolojia ya ujenzi wa madaraja kwa kutumia mawe na
matofali ya kuchoma pamoja na ujenzi wa barabara kwa kutumia mawe ilikuja baada
ya kuwa na mtandao mkubwa wa barabara na hivyo kuweza kutumia teknolojia hiyo
ili kupunguza gharama za ujenzi.
“Ulinganifu wa barabara zetu zina mtandao wa Km 144,429.77,
mtandao huu ni mkubwa sana hivyo tuliona tutumie teknolojia hii ya mawe ili
tuweze kuwafungulia njia wananchi kuweza kufika maeneo yao ya huduma za jamii.”
Ameongeza kuwa tangia mwaka 2017 hadi sasa TARURA imeweza
kujenga madaraja 212 yenye gharama ya shilingi Bilioni 8.2 na kama wangejenga
kwa kutumia zege wangetumia zaidi ya shilingi 36. “Teknolojia hiyo imeweza
kupungunguza gharama mpaka asilimia 80.”
Aidha, amesema mawe pamoja na matofali wanayoyatumia hupimwa
maabara na kiwango cha chini cha ugumu wa mawe (MPA) huwa zaidi ya 25 na
matofali ‘MPA’8 ndio hujengea madaraja.
Naye, Rais wa Taasisi ya Wahandisi Tanzania (IET) Mhandisi
Dkt. Gemma Modu alisema Uhandisi una mchango mkubwa wakuleta maendeleo nchini.
Pia ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na
Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuongeza kasi ya maendeleo nchini na kuongeza
wahandisi wazawa na kuwafungulia fursa wahandisi na mafundi na kuahidi
kushirikiana bega kwa bega na Serikali.
Na. Catherine Sungura- Arusha
0 Maoni