Jeshi la Polisi nchini limeyazuia mabasi matano ya abiria
katika Stendi Kuu ya Mabasi Jijini Mbeya kujendelea na safari baada ya kukutwa
na changamoto katika mifumo mbalimbali.
Akizungumza mapema leo Desemba 26, 2023 Mwanasheria Mkuu wa
Kikosi cha Usalama barabarani nchini, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Deus Sokoni
baada ya kuendesha zoezi la ukaguzi wa mabasi, Uuimaji wa kilevi kwa madereva
na utoaji wa elimu katika Stendi hiyo amesema, jumla ya mabasi ya abiria 58
yamekaguliwa ambapo kati ya hayo mabasi Matano kutoka kampeni ya TURU BEST,
ISAMILO EXPRESS, ARUSHA EXPRESS, MSIGWA na AHMED yalikutwa na hitilafu katika
mifumo mbalimbali ikiwemo mfumo wa breki.
“Jeshi la Polisi nchini kwa kushirikiana na mamlaka nyingine
kama vile mamlaka ya udhibiti wa usafiri ardhini (LATRA) limepewa mamlaka ya
kuzuia chombo cha moto kuendelea na safari pindi linapofanya ukaguzi na
kugundua changamoto ikiwemo ubovu na hitilafu katika mifumo ya chombo hicho”
alisema Mrakibu Mwandamizi Sokoni.
Aidha, Afisa Leseni kutoka mamlaka ya udhibiti wa usafiri ardhini ndugu Amani Masuwe amesema kuwa, wamefanya jitihada mbalimbali kuhakikisha abiria waliokuwa wasafiri na mabasi hayo wanapata usafiri mwingine na wengine kurudishiwa nauli zao ili kufanya utaratibu wa safari kwa siku nyingine.
Naye, Balozi wa usalama barabarani Mkoa wa Mbeya ndugu Yonna
Mleka amewataka madereva kujenga utamaduni wa kufanya ukaguzi wa magari yao
kabla ya kuanza safari ili kuepuka usumbufu kwao nak wa abiria wanaowasafrisha
Pamoja na kuepuka madhara mengine wawapo safarini.
Ameongeza kuwa, Mabalozi wa usalama barabarani wataendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi na mamlaka nyingine kutoa elimu kwa abiria kupitia kampeni ya Abiria Paza Sauti (APS), kukemea na kutoa taarifa za madereva wanaokiuka sheria za usalama barabarani na kuhatarisha usalama wa abiria na watumiaji wengine wa Barabara.
0 Maoni