RC Chalamila ahimiza uadilifu kwa watendaji wa kata na mitaa

 

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila amewataka watendaji wa kata na mitaa kuwa waadilifu wakati wote wanapotekeleza majukumu yao kwa kuwa wanaishi na jamii moja kwa moja vile vile miradi mingi ya mendeleo inatekelelezwa katika ngazi ya Kata au mtaa

RC Chalamila ameyasema jana wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya maafisa Tarafa na watendaji wa kata wa mkoa wa Dar es salaam uliofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke yatakayofanyika kwa siku mbili kuanzia jana hadi leo Novemba 24,2023.

Vilevile amesema watumishi wanapaswa kuwa na maadili ili kuleta picha nzuri kwa wananchi ikiwa wakiharibu lawama za wananchi zinaenda moja kwa moja kwa viongozi wa juu.

Aidha, Mhe. Chalamila amewataka watumishi hao waelewe uadilifu si umaskini na utajiri si wizi, "Kuna utofauti mkubwa kati ya uadilifu na umaskini na wengi wanadhani muadilifu ni kuwa maskini, kwahiyo acheni kuishi kimaskini ili muonekane ni waadilifu."

Pia RC Chalamila amesema mafunzo hayo yana umuhimu mkubwa sana na aliwaasa viongozi hao kutatua kero na changamoto za wananchi ikiwemo migogoro ya ardhi, kusimamia amani na usalama wao, usimamizi mzuri wa miradi na pesa wanazokabidhiwa zitumike kama zilivyopangiwa, wajiepushe na vitendo vya rushwa na kuwadhulumu wanyonge haki zao.

Naye Mkuu wa wilaya ya Temeke Mhe Sixtus Mapunda alisema mafunzo ni mama wa uelewa wa mambo yote na kuhimiza yawe yanatolewa mara kwa mara ili kuzidi kuwajengea uwezo na kutambua nafasi zao kama watumishi sababu wao ndiyo wapo karibu zaidi na wananchi na kutambua kero na changamoto zao.

Kwa upande wa mwenyekiti wa mafunzo hayo Hulda J. Ulomi alitoa neno la shukrani kwa Mhe Chalamila kwa kufunguzi na maelezo yake, na kuahidi kwamba watafuatilia mafunzo yote kwa umakini na kwenda kuwa bora zaidi katika utendaji wa majukumu yao.

Chapisha Maoni

0 Maoni