Mkazi wa Lumala wilayani Ilemela mkoani Mwanza, Salma
Abdallah (37), amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya hiyo na kusomewa shtaka la
kujihusisha na matumizi ya dawa za kulevya aina ya bangi.
Salma amesomewa shtaka hilo katika kesi ya Jinai namba
152/2023 ambapo anadaiwa kutenda kosa hilo kinyume na Kifungu namba 17 (1) (b)
cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Madawa ya Kulevya Sura ya 95 toleo la
Mwaka 2019.
Akimsomea shtaka hilo mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi wa
mahakama hiyo, Amani Sumari, Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Monika Mweli
amesema mshtakiwa alitenda kosa hilo kati ya tarehe 1.10.2023 na tarehe
27.10.2023, eneo la Lumala Wilaya ya Ilemela.
Baada ya kusomewa shtaka hilo, mshatakiwa amekana na
kurejeshwa rumande kutokana na kutokidhi masharti ya dhamana ambapo alitakiwa
kuwa na wadhamini wawili na kila mmoja kusaini bondi ya maneno ya shilingi
milioni mbili kwa kila mmoja, kitambulisho pamoja na barua ya mwenyekiti wa
serikali ya mtaa ambapo mshtakiwa alijibu hana wadhamini hao.
Hakimu, Sumari ameahirisha shauri hilo hadi tarehe
13.11.2023 litakapokuja kwa ajili ya mshtakiwa kusomewa maelezo ya awali ya
shtaka linalomkabili.
0 Maoni