Muhimbili kushirikiana na China kuboresha huduma za upandikizaji viungo

 

Uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili umekutana na ujumbe kutoka Jimbo la Shandong nchini China na kujadiliana namna ya kushirikiana ili kuendelea kuboresha huduma za kibingwa na kibobezi sambamba na kuwajengea uwezo wataalamu.

Ujumbe huo umeongozwa na Kiongozi Mkuu wa Afya wa Jimbo la Shandong Bi. Ma Lixin umetembelea maeneo mbalimbali ya kutolea huduma ikiwemo Idara ya Magonjwa ya Dharura kwa upande wa watoto na wodi ya wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum (ICU).

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa MNH, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Dkt. Julieth Magandi amesema kwasasa MNH inapenda ishirikiane katika maeneo ya ICU, magonjwa ya dharura, upandikizaji wa viungo ikiwemo ini, uloto na figo.

“Tayari upandikizaji wa figo tunafanya, mpaka sasa tumepandikiza figo wagonjwa 88 ambapo kati ya hao 81 wamepandikizwa Muhimbili Upanga na wengine 7 wamepandikizwa Muhimbili Mloganzila. Hata hivyo kwa upande wa upandikizaji figo tunahitaji kujengewa uwezo katika upasuaji mkubwa zaidi kwani upandikizaji wa kawaida tunafanya,” amesema Dkt. Magandi.

 “Serikali ya Tanzania inayoongozwa na Mh. Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya kuanzia ngazi ya chini hadi taifa kwa kuweka vifaa tiba vya kisasa, kwa mfano hapa Muhimbili tunavifaa vya kisasa vya kufanyia uchunguzi na tiba ikiwemo MRI, Angio Suite, Digital X-Ray na CT-Scan pamoja na vingine vingi hii yote ni kuhakikisha huduma za kibingwa na kibobezi zinapatikana hapa hapa nchini,” amefafanua Dkt. Magandi.

Naye Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Tiba Asili na muwakilishi kutoka Wizara ya Afya Dkt. Vumilia Luggyle amesema Tanzania imepiga hatua kwenye utalii tiba ambapo inahudumia watu kutoka mataifa mbalimbali Afrika ikiwemo Zambia, Kenya, Zimbabwe, Malawi, Uganda hivyo kuna umuhimu kwa nchi hizi mbili kushirikiana.

Kwa Upande wake Kiongozi Mkuu Sekta ya Afya Jimbo la Shandong Bi. Ma Lixin amefurahishwa na namna ambavyo Muhimbili imepiga hatua katika utoaji wa huduma za fya hususani za kibingwa na kibobezi na kuahidi kushirikiana ili kuendelelea kuleta matokeo chanja katika sekta ya afya.

Chapisha Maoni

0 Maoni