Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe amewataka Maafisa Ugani kutumia taaluma zao vizuri ili kusaidia kutimiza malengo ya Serikali ya Awamu ya sita inayoongozwa na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuhakikisha Sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi zinazalisha vya kutosha na kuiwezesha nchi kuwa kapu la Chakula Barani Afrika.
Prof. Shemdoe amesema hayo
wakati akifungua Kongamano na Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Maafisa Ugani
nchini (TSAEE) kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega
unaofanyika jijini Dodoma kuanzia jana Novemba 20 hadi leo tarehe 21, 2023.
"Nyinyi ndio injini,
hivyo katika Mkutano wenu huu jielekezeni katika kutimiza malengo ya Serikali
ya Awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan ambayo imeweka
kipaumbele katika kuhakikisha sekta hizi zinachangia katika upatikanaji wa
chakula, lishe na kukuza kipato cha Wananchi ambao zaidi ya Asilimia 65
wanajishughulisha na Kilimo, Mifugo na Uvuvi", alisema Prof. Shemdoe.
Aliongeza kuwa kutokana na
umuhimu wa Sekta hizo Serikali imekuwa ikiongeza bajeti kila mwaka lengo likiwa
kuleta mageuzi katika Sekta ya Kilimo kwa kuongeza tija kwenye uzalishaji,
kuimarisha usalama wa chakula na lishe; Kuimarisha upatikanaji wa masoko,
mitaji na kuongeza mauzo ya bidhaa za kilimo, mifugo na uvuvi ndani na nje ya
nchi.
Aliendelea kusema kuwa
Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo wa ndani na nje ya nchi
ambao wanaonesha dhamira ya dhati ya kuungana na serikali katika kuhakikisha
Tanzania inafikia uchumi wa kati kupitia shughuli za kilimo, ufugaji na uvuvi.
Aidha, aliwataka Maafisa
Ugani hao kuhakikisha wanatoa ushirikiano wa kutosha kwenye mradi wa kielelezo
wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan wa Jenga Kesho Iliyobora (BBT).
"Nyinyi ndio washauri
wa kwanza katika programu ya BBT ambayo imelenga kuwainua vijana, utaalamu wenu
utasaidia kutimiza malengo ya Rais, Dkt. Samia ya kuwainua vijana na kina mama
hapa nchini", alibainisha.
Naye, Mwenyekiti wa Chama
cha Maafisa Ugani (TSAEE), Prof. Catherine Msuya alizishukuru Wizara za kisekta
kwa kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili Maafisa Ugani huku akiomba
Wizara hizo ziendelea kukilea chama hicho kwa kukitengea bajeti ili chama hicho
kiweze kujiendesha bila matatizo.
Halikadhalika, aliziomba
Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Kilimo na TAMISEMI kuboresha na kuweka mfumo mmoja
ambapo utawawezeaha Maafisa Ugani hao kuwasiliana vyema tofauti na ilivyo sasa
ambapo kuna mifumo mingi tofautitofauti.
0 Maoni