Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila amepokea vifaa tiba vya msaada uliotolewa na Shirika la DKT international ambavyo ameelekeza vipelekwe katika Wilaya ya Kigamboni na Ubungo za Jijini Dar es Salaam.
Akipokea msaada huo wa vifaa tiba RC Chalamila amelishukuru shirika
hilo kwa kuunga mkono juhudi za Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika kuboresha
sekta ya Afya hapa nchini, mchango uliotolewa ni wa thamani kubwa, ametoa rai
kwa wadau wengine wa afya katika mkoa kuiga mfano na kuunga mkono juhudi za
Serikali katika katika mkoa.
"Rais Dkt Samia Suluhu amekuwa akitoa pesa nyingi na
anaendelea kutoa katika kuboresha sekta ya afya, ujenzi wa vituo vya afya,
zahanati na hospitali zimeendelea kujengwa kila kona hivyo kuunga mkono juhudi
hizi ni kumpa nguvu Rais aendelee kupambana zaidi kwa masilahi mapana ya
Watanzania," alisema RC Chalamila.
Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa wa Dar es Salaam amewataka wahusika
wa Wilaya ya Ubungo na Kigamboni kuhakikisha wanavitunza vifaa tiba walivyopatiwa
ili viweze kutumika kwa muda mrefu kwa manufaa ya umma.
Kwa upande wa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt
Rashid Mfaume ameanisha vifaa tiba vilivyotolewa na Shirika la DKT
International ikiwemo vitanda kwa ajili ya operesheni, makabati na viti mwendo,
pia amewaomba kuendeleza ushirikiano na mkoa katika kutekeleza afua mbalimbali
za kukabiliana na magonjwa ya ngono, uzazi wa mpango na Ukimwi.
DKT International ni shirika lisilo la Kiserikali ambalo
linajishughulisha zaidi na upangaji uzazi, kuzuia VVU/UKIMWI na uzuiaji mimba
kwa njia salama.
0 Maoni