Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia
Suluhu Hassan amesema ifikapo mwaka 2024 Mkoa wa Singida hautashuka 97 % ya
upatikanaji wa umeme mkoani Singida.
Mhe. Rais amesema hayo alipokuwa Mgeni Rasmi katika
madhimisho ya Miaka 60 ya kuanzishwa kwa Mkoa wa Singida yaliyofanyika katika
viwanja vya Bombadia tarehe 16 Oktoba, 2023 mkoani humo.
“Kwa upande wa Umeme, Naibu Waziri wa Nishati amesema hapa
ikifika Desemba mwaka ujao, kama sio 100%, hatutashuka 97% ya upatikanaji wa
umeme ndani ya Singida,”alisema Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith
Kapinga, amesema Serikali imetoa shilingi Bilioni 72 kwa ajili ya kuvipatia
vijiji vyote 171 ambavyo vilikuwa havijapatiwa umeme ambapo mpaka sasa Vijiji
50 vilivyobakia wakandarasi wako site wanaendelea na kazi.
Pamoja na miradi ya kusambaza umeme amesema Serikali imetoa
fedha kwa ajili ya kupeleka umeme kwenye maeneo ya kimkakati ili kuboresha
uchumi wa watu wa Singida
Serikali imetoa shilingi Bilioni 7 kwa ajili ya kupelekea
umeme katika maeneo ya Pembezoni mwa Miji (Peri-Urban III) katika maeneo 34.
Vilevile mradi wa kupeleka umeme kwenye Mabwawa ya
umwagiliaji na migodi midogo 22 kwa gharama ya shilingi Bilioni 5 kwa ajili ya
kuinua uchumi wa wananchi wa mkoa huo.
Na. Zuena Msuya na Mayloyce Mpombo- Singida
0 Maoni