Rais Samia aahidi umeme wa uhakika Singida 2024

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema ifikapo mwaka 2024 Mkoa wa Singida hautashuka 97 % ya upatikanaji wa umeme mkoani Singida.

Mhe. Rais amesema hayo alipokuwa Mgeni Rasmi katika madhimisho ya Miaka 60 ya kuanzishwa kwa Mkoa wa Singida yaliyofanyika katika viwanja vya Bombadia tarehe 16 Oktoba, 2023 mkoani humo.

“Kwa upande wa Umeme, Naibu Waziri wa Nishati amesema hapa ikifika Desemba mwaka ujao, kama sio 100%, hatutashuka 97% ya upatikanaji wa umeme ndani ya Singida,”alisema Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga, amesema Serikali imetoa shilingi Bilioni 72 kwa ajili ya kuvipatia vijiji vyote 171 ambavyo vilikuwa havijapatiwa umeme ambapo mpaka sasa Vijiji 50 vilivyobakia wakandarasi wako site wanaendelea na kazi.

Pamoja na miradi ya kusambaza umeme amesema Serikali imetoa fedha kwa ajili ya kupeleka umeme kwenye maeneo ya kimkakati ili kuboresha uchumi wa watu wa Singida

Serikali imetoa shilingi Bilioni 7 kwa ajili ya kupelekea umeme katika maeneo ya Pembezoni mwa Miji (Peri-Urban III) katika maeneo 34.

Vilevile mradi wa kupeleka umeme kwenye Mabwawa ya umwagiliaji na migodi midogo 22 kwa gharama ya shilingi Bilioni 5 kwa ajili ya kuinua uchumi wa wananchi wa mkoa huo.

Na. Zuena Msuya na Mayloyce Mpombo- Singida

Chapisha Maoni

0 Maoni