Rais Dk. Mwinyi ayataka mashirika ya umma kukuza uchumi wa kidijitali

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi ametoa rai kwa mashirika ya utangazaji ya umma kuwekeza na kuwa na vitendea kazi vya kisasa vinavyoendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia duniani katika ukuaji wa uchumi wa kidijitali kwa maendeleo endelevu.

Rais Dk. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 10 Oktoba 2023 wakati alipofungua mkutano mkuu wa 30 wa mashirika ya utangazaji ya umma kutoka nchi za Kusini mwa Afrika (SABA) uliofanyika ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip Airport, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Aidha Rais Dk. Mwinyi ameeleza kuwa ni wakati sahihi kuhakikisha vyombo vya utangazaji vya umma vinakuwa na vyanzo vya uhakika vya mapato vihimili changamoto za kifedha kwa kutimiza ipasavyo dhana ya kukuza, kulinda na kutangaza utamaduni wa mwafrika.

Halikadhalika Rais Dk. Mwinyi amewakaribisha wajumbe wa mkutano huo kutembelea vivutio vya utalii vinavyopatikana Zanzibar ikiwemo urithi wa dunia wa Mji Mkongwe pia na vivutio vya upande wa Tanzania bara ikiwemo Mlima wa Kilimanjaro, Hifadhi za Taifa za Serengeti, Ngorongoro na Manyara.

Mkutano huo wa siku tatu utajadiliana kwa kina nafasi ya TEHAMA na mchango wake katika ukuaji wa uchumi wa kidijitali Afrika ili kuleta maendeleo endelevu.

Chapisha Maoni

0 Maoni