Watoto 45 wenye magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo yakiwemo
matundu kwenye moyo, na matatizo ya mishipa ya damu kufanyiwa upasuaji wa moyo
katika kambi maalum inayofanywa na wataalamu wa afya wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao kutoka Shirika la Mending Kids
lililopo nchini Marekani.
Kambi hiyo maalumu ya siku tano iliyoanza jana inatarajiwa
kutoa matibabu ya upasuaji wa moyo wa tundu dogo kwa kutumia mtambo wa cathlab
kwa watoto 25 na upasuaji mkubwa wa moyo wa kufungua kifua kwa watoto 20.
Akizungumza na mwandishi wa habari hii Daktari bingwa wa
magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Stella
Mongela alisema upande wa cathlab watoto 25 watapatiwa matibabu ya kuziba
matundu mbalimbali yaliyopo katika kuta za moyo pamoja na kufungua mishipa ya
damu iliyobana inayopeleka damu kwenye mapafu na kwenye mwili.
Dkt. Stella alisema kupitia kambi mbalimbali zinazofanyika
JKCI zimekuwa zikitoa fursa kwa madaktari wazawa kuendeleza ujuzi wao kwani
wamekuwa wakikutana na mabingwa waliofanya kazi kwa muda mrefu hivyo kuongeza
ujuzi zaidi.
“Kambi ya wataalamu wa afya kutoka Shirika la Mending Kids
ni moja ya kambi inayotupa nafasa wataalamu wa JKCI kujifunza mbinu mbalimbali
za kutoa huduma bora za matibabu ya magonjwa ya moyo kwa watoto,” alisema Dkt.
Stella.
Kwa upande wake Daktari bingwa wa upasuaji mkubwa wa moyo
kwa watoto kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Felix Shonyela alisema
Idara ya upasaji mkubwa wa moyo imepanga kuwafanyia upasuaji wa moyo watoto
kati ya watatu hadi wanne kila siku wakati wa kambi hiyo maalumu.
Dkt. Shonyela alisema wakati wa kambi maalumu watafanya
upasuaji wa moyo kwa watoto wenye magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo yakiwemo
matundu katika moyo na mishipa ya damu ambayo haiko sawa inayopeleka damu
kwenye mapafu.
“Katika kambi hii tutaenda kurekebisha mishipa ya damu
ambayo haiko sawa inayoelekea kwenye mapafu na kupelekea mishipa mingine
inayochukua damu kutoka kwenye moyo kwenda kwenye mapafu kuwa midogo,
tunarekebisha mishipa hiyo ili damu iweze kwenda vizuri kwenye mapafu,” alisema
Dkt. Shonyela.
0 Maoni