Kasi ya ujenzi wa miundombinu ya Hifadhi ya Taifa Ruaha yaridhisha

 

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Kamishna Benedict Wakulyamba ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa miundombinu ya utalii inayotekelezwa na Mradi wa REGROW ndani ya Hifadhi ya Taifa Ruaha.

Kamishna Wakulyamba ameyasema hayo katikati ya wiki hii alipofanya ziara ya kikazi Hifadhi ya Taifa Ruaha iliyopo mkoani Iringa, ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na REGROW katika Hifadhi za Taifa Ruaha, Mikumi na katika kijiji cha Madibila kilichopo wilayani Mbarali.

"Nimeridhishwa na kasi ya ujenzi wa miundombinu inayoendelea kujengwa, natarajia itakapokamilika itapunguza changamoto zilizokuwepo, pia itaongeza idadi ya watalii watakaoitembelea hifadhi hii ambayo nimeambiwa ni ya pili kwa ukubwa Tanzania".

"Niwashukuru wenzetu wa Benki ya Dunia kwa kutupatia msaada huu ili tuboreshe miundombinu ya utalii, uwanja huu ukikamilika utakuwa na uwezo wa kushusha ndege za wastani zenye uwezo wa kubeba watalii 48. Mathalani, ikishusha Ruaha, baadae Mikumi na Nyerere itawarahisishia watalii kutembelea hifadhi nyingi zaidi kwa siku chache lakini mapato yakiongezeka zaidi kwa taifa", aliongeza Kamishna Wakulyamba.

Sambamba na hilo pia, Kamishna wakulyamba alifanya kikao na maafisa na askari wa Hifadhi ya Taifa Ruaha na kuwataka kuwa na nidhamu na uadilifu katika utendaji kazi wao, alisema "msingi wa jeshi lolote ni nidhamu cha pili kinachofanana na hicho ni uadilifu na ukiviangalia vyote viwili ni lazima ule kiapo, hivyo ni wajibu wenu kuyaishi na kuyatenda."

Naibu Kamishna wa Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara Herman Batiho, aliahidi TANAPA kuisimamia na kuilinda miradi hiyo ili ikamilike kwa wakati.

"Miradi hii ikikamilika kwa viwango tunavyokusudia itaiwezesha serikali na hifadhi hii kukuza utalii Kanda ya Kusini na kuongeza pato la Taifa kupitia shughuli za utalii na miradi mingine ya umwagiliaji inayohudumia jamii," aliongeza Kamishna Batiho.

Kamanda wa Uhifadhi Kanda ya Kusini, Steria Ndaga alimpongeza Kamishna Wakulyamba kwa kukagua miradi na kuongea na watumishi alisema, "kwa kipindi kifupi tangu uteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan umetembele hifadhi za Kanda ya Kusini zote, ukikagua miradi na kuongea na watumishi, tunakuahidi maelekezo yote uliyatoa kwetu tutayatekeleza na kuyaishi."

Miradi inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na ujenzi wa viwanja vya ndege viwili, nyumba kwa ajili ya malazi kwa wageni (cottages) zenye vitanda 176 na kituo cha kutoa taarifa za utalii kwa wageni (Visitors Information Centre).

Na. Jacob Kasiri- Ruaha.

Chapisha Maoni

0 Maoni