Mganga Mkuu Mkoa wa Rukwa Dkt. Ibrahim Isack ameipongeza
Wizara ya Afya pamoja na wadau mbalimbali ikiwemo Shirika la Afya Duniani (WHO),
Shirika la Kuhudumia Watoto Duniani (UNICEF) pamoja na Save the Children kwa
kuweka nguvu za pamoja kufanikisha Kampeni ya Chanjo ya Matone dhidi ya Polio.
Dkt. Isack ametoa pongezi hizo Mkoani Rukwa ikiwa Uzinduzi
wa Kampeni ya Chanjo ya Matone dhidi ya Polio kitaifa ulifanyika Mkoani humo
huku walengwa ilikuwa ni watoto walio na umri chini ya miaka 8 katika mikoa 6 ya
Rukwa, Katavi, Kagera, Kigoma, Mbeya na Songwe.
"Kwa kweli Wizara ya Afya pamoja na wadau ikiwemo WHO,
UNICEF na Save the Children wamekuwa na mchango mkubwa hususan suala uwezeshaji
na uelimishaji kwa jamii," alisema Dkt. Isack.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Sumbawanga Mkoani
Rukwa Catherine Mashalla amesema hamasa ya Elimu ya Afya kwa Umma imekuwa na
mchango mkubwa kufikia jamii kupata chanjo ya Polio kwa watoto.
"Tunashukuru tumekuwa tukihamasisha jamii na Elimu ya
Afya kwa Umma pamoja na Mpango wa Taifa wa Chanjo wametusaidia sana kupita
sehemu mbalimbali na kutumia wimbo wa hamasa," alisema Mashalla.
Mratibu wa Chanjo Mkoa wa Rukwa Ndenisia Ulomi amesema wadau
wamesaidia katika ufuatiliaji wa magonjwa yanayozuilika kwa chanjo ambapo jumla
ya watoto 546, 026 wamepatiwa chanjo Mkoani Rukwa.
"Tumeshirikiana na Wizara ya Afya pamoja na Wadau
ambapo katika halmashauri ya Wilaya ya Kalambo lengo ilikuwa ni kuchanja watoto
80,486 waliofikiwa ni watoto 111,524
sawa na asilimia (138.56%), Nkasi DC
lengo ni kuchanja watoto 109,514 na
waliochanjwa ni watoto 145, 234 sawa na asilimia 132.62%, Sumbawanga DC lengo
ni watoto 118,071 na waliochanjwa ni watoto 175,165 sawa na 148.36% na
Sumbawanga MC lengo lilikuwa watoto 83,811 na waliochanjwa ni watoto 114,103
sawa na asilimia 136.14%,"alisema Ulomi.
Naye mwakilishi wa Save the Children George Sungwa amesema
Wizara ya Afya, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Mkoa wa Rukwa pamoja na wadau wengine
wamekuwa na mchango mkubwa katika Kampeni ya Polio.
Alex Mwembezi pamoja na Rusia Swaila ni miongoni mwa wakazi
wa Mkoa wa Rukwa ambapo wamesema kutokana na hamasa ya Elimu ya Afya kwa Umma
wamekuwa na uelewa juu ya chanjo ya matone dhidi ya ugonjwa wa Polio ikiwemo
kuzuia kupooza.
Ikumbukwe kuwa Kampeni ya chanjo ya matone dhidi ya ugonjwa
wa Polio ilianza Septemba 21-24, 2023 katika mikoa 6 ya Rukwa, Kagera, Katavi,
Kigoma, Mbeya na Songwe na matarajio ya kuchanja ni zaidi ya watoto milioni
tatu.
0 Maoni