TFF yafafanua Waziri Ndumbaro aliondolewa adhabu ya kifungo

 

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limetoa ufafanuzi kuhusiana na taarifa zilizoenea mitandaoni kuhusu kufungiwa kwa Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Damas Ndumbaro aliyehamishiwa hivi karibuni na rais kushika wadhifa huo.

Taarifa iliyotolewa leo Dar es Salaam na Ofisa Habari na Mawasiliano wa TFF, Cliford Ndimbo, imesema kwamba usahihi ni kuwa Waziri Dk. Ndumbaro alifungiwa miaka saba na uongozi wa TFF uliopita.

Ndimbo amesema kwamba hata hivyo, Dk. Ndumbaro hakukubaliana na uamuzi huo, ambapo alikata rufani katika Kamati ya Rufani ya Nidhamu ya TFF kupinga adhabu hiyo.

Amesema kwamba, Kamati ya Rufani ya Nidhamu ya TFF chini ya uongozi wa sasa ilisikiliza rufani hiyo mwaka 2017, ambapo Waziri Ndumbaro alishinda, na kuondolewa adhabu ya kufungiwa.

Katika taarifa hiyo, Ndimbo amemalizia kwa kusema kwamba kwa sasa Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Dk. Damas Ndumbaro, ni Mwenyekiti wa Kamati ya Rufani ya Leseni ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Chapisha Maoni

0 Maoni