Sio kweli, Ngorongoro haisafirishi nje ya nchi wanyamapori- NCAA

 

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), imekanusha taarifa zinazosambazwa kuhusu madai ya usafirishaji wa wanyamapori nje ya nchi kupitia maeneo ya Hifadhi ya Ngorongoro na Pori la Akiba la Pololeti.

Katika taarifa yake, Mkuu wa Kitengo cha Uhusianao kwa Umma wa mamlaka hiyo Joyce Mgaya amesema kwamba taarifa zinazosambazwa kupitia baadhi ya mitandao ya kijamii kuhusu usafirishaji wa wanyamapori kwa kutumia ndege za mizigo sio za kweli.

Aidha, amesema kwamba wawekezaji wote waliopo katika eneo la Hifadhi ya Ngorongoro na Pori la Akiba la Pololeti, wakiwemo kutoka Falme za Kiarabu (UAE) na Marekani huendesha shughuli zao za utalii wa picha na uwindaji kwa mujibu wa sheria za nchi.

"Ikumbukwe kwamba eneo la Hifadhi ya Ngorongoro ni moja ya maeneo ya Urithi wa Dunia chini ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO), na hutazamwa na taasisi zote ndani na nje ya nchi ambazo husimamia shughuli za uhifadhi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu," amesema Joyce.

Bi. Joyce amesema kwamba kutokana na sifa hizo, maeneo hayo ya hifadhi hayajawahi kuwa maeneo ya kusafirisha wanyamapori wala kukiuka misingi ya shughuli za uhifadhi wa rasilimali hizo za taifa.

Amemalizia taarifa yake hiyo kwa kuwaomba wananchi wapuuze taarifa hizo, kwani sio za kweli na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro inaendelea kutekeleza majukumu yake ya uhifadhi, utalii na maendeleo ya jamii.

Chapisha Maoni

0 Maoni