Tanzania kuzalisha dawa ya kuulia wadudu wa mazao isiyo na sumu

 

Tanzania kuanza kuzalisha kwa mara ya kwanza dawa ya kuulia wadudu isiyokuwa na sumu katika kiwanda cha Viuadudu cha Tanzania Biotech Products Limited kilichopo Kibaha katika mkoa wa Pwani kinachomilikiwa na Shirika la Maendeleo ya Taifa (NDC).

Akiongea katika video fupi aliyoituma kutoka Jijini Havana, Balozi wa Tanzania nchini Cuba, Humphrey Polepole, amesema tayari wameshampata mtaalamu bingwa na mbobezi kutoka Cuba na wiki ijayo atakuja nchini kwa ajili ya kazi hiyo.

“Tayari tumeshapitia nyaraka zake na wiki ijayo mimi mwenyewe nitamsindikiza uwanja wa ndege kuhakikisha anakuja nyumbani kwetu Tanzania, na huyu ni mtaalamu tutamuweka katika kiwanda chetu cha kutengeneza viuadudu pale Kibaha kwa ajili ya kuzalisha dawa hiyo,” alisema Balozi Polepole.

Amesema kwa sasa, uzoefu ni kwamba tunapulizia sumu ili kuua wadudu wanaoshambulia mazao katika mahindi, maharage, pamba na aina zote za mazao, ila sasa kwa mara ya kwanza nchini Tanzania itaanza uzalishaji wa dawa ya kuua wadudu isiyo na sumu aina ya Bio Pesticides.

“Zama za kupulizia sumu kuulia wadudu kupata magonjwa ya kansa na magonjwa ya ngozi na kila kitu zimekwisha, tutumie dawa hii ya kuulia wadudu wanaoharibu mazao ambayo sio sumu,” alisema Balozi Polepole na kuongeza “Dawa hii imethibitika na cheti imeshapata kutoka Tanzania inatambulika na inafanya vizuri zaidi kuliko dawa zenye sumu, achana na sumu tumia Bio Pesticides, tunataka kuanza katika msimu huu afya kwa Watanzania. “

Chapisha Maoni

0 Maoni