NCAA na JKT wasaini mkataba ujenzi wa nyumba 5,000 za wanaohama Ngorongoro

 

Serikali kupitia Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) imesaini mkataba wa Makubaliano na Jeshi la Kujenga Taifa kupitia SUMA- JKT kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Nyumba 5,000 za Wananchi wanaoishi katika hifadhi ya Ngorongoro ambao wanaendelea kujiandikisha kwa ajili ya kuhama kwa hiari.

Kwa mujibu wa Kamiahna wa Uhifadhi wa NCAA Dkt. Freddy Manongi Mradi wa ujenzi wa nyumba hizo 5,000 unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba, 2023 na tayari Serikali imeshatenga Shilingi bilioni 97 ambapo mradi huo unatarajia kukamilika katika kipindi cha miezi sita ijayo.

Katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa zoezi hilo nyumba zaidi ya 500 zilijengwa na tangu zoezi hilo lilipoanza mwezi Juni, 2022, tayari makundi 19 yenye kaya zaidi ya 565 watu 3097 na mifugo zaidi ya 15,500 imeshahama ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro.

Hamasa ya wananchi kujiandikisha kuhama kwa hiari imeendelea kuongezeka na hadi sasa jumla ya Kaya 1524 zimeshajiandikisha kuhama kwa hiari.

Kamishna Manongi ameeleza kuwa katika utekelezaji wa awamu inayofuata pamoja na wananchi kuhamishiwa Nyumba zinazojengwa na Serikali lakini wananchi watapewa uhuru wa kuhamia mahali popote wanapotaka na Serikali itawapa stahiki zao kwa mujibu wa sheria.

Serikali itaendelea kuhamisha wakazi wa Ngorongoro walioomba kuhama kwa hiari kwa kuzingatia mizingi ya haki za kibinadamu.

Na. Kassim Nyaki- Arusha

Chapisha Maoni

0 Maoni