Watu wawili akiwemo raia wa Burundi Niyokindi Anthony (44),
wamehukumiwa kutumikia kifungo cha miaka sita gerezani baada ya kukiri kutenda
kosa la kuvunja Ofisi ya Mganga Mkuu wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza na kuiba
pikipiki tatu zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni kumi na moja huku
mmoja akikana shtaka na kurudishwa rumande kwa kukosa dhamana
Mbali na raia wa Burundi mwingine aliyehukumiwa kutumikia
kifungo hicho ni mkazi wa Isungangh'olo wilayani Sengerema Ibrahim Mshengezi
(55) ambapo wamehukumiwa kwa kutenda makosa mawili ambayo ni kuvunja ofisi na
kuiba kinyume na vifungu 297 na 258 vya Kanuni ya Adhabu sura ya 16
iliyofanyiwa marejeo mwaka 2022.
Katika kesi hiyo yenye washtakiwa watatu, mshtakiwa mwingine
ambaye ni Mkazi wa Isungangh'olo wilayani Sengerema, Anold Paul (25) amekana
mashtaka hayo ambapo Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama hiyo, Evod Kisoka
ameamuru arejeshwe rumande baada ya kukosa wadhamini
Awali, akiwasomea maelezo ya kosa washtakiwa, Mwendesha
Mashtaka wa Serikali, Sajenti wa Polisi Theophilius Bei alisema washtakiwa
walitenda makosa hayo Agosti 20 mwaka huu kwa kuiba pikipiki tatu za Serikali
zenye namba ya usajili, SM15342, SM15343 na SM15349, zote kampuni ya Yamaha
kinyume na Kanuni ya adhabu Sura ya 16 toleo la mwaka 2022.
Hata hivyo, shtaka dhidi ya mshtakiwa namba tatu (Anold
Paul) ambaye amekana mashtaka hayo litaendelea tarehe 2/10/2023.
Hakimu Kisoka amesema Mahakama inatoa hukumu ya miaka sita
kwa washtakiwa ili iwe funzo kwa wengine.
CHANZO: Mimi Online Tv
0 Maoni