Wamiliki wa Makao ya watoto wametakiwa kuhakikisha wanatoa
huduma kwa mujibu wa sheria na kanuni na kuhakikisha rasilimali zinazopatikana
kwa ajili ya kusaidia watoto zinatumika kikamilifu kwa maendeleo na ustawi wa
watoto.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia,
Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima wakati akifungua Mkutano
wa Wamiliki wa Makao ya Watoto Mkoa wa Dar es Salaam Agosti 04, 2023.
Dkt. Gwajima amebainisha kwamba, pamoja na makao mengi
kufanya kazi nzuri na kwa uwazi, baadhi yamekuwa yakikusanya rasilimali na
kujinufaisha wao zaidi kuliko walengwa ambao ni watoto walioko kwenye vituo
hivyo huku wamiliki wa baadhi ya makao hayo wakiwazuia na kuwapa vitisho
Maafisa Ustawi wa Jamii pale wanapofika kwenye makao hayo kufanya ufuatiliaji
na ukaguzi wa utoaji wa huduma.
"Jambo hilo ni kosa kisheria kwa mujibu wa Kifungu cha
146 (2) (c) na adhabu yake ni kifungo kisichopungua mwaka mmoja au faini
isiyopungua milioni 2 na isiyozidi milioni 10 au vyote viwili na pia ofisi ya
msajili inaweza kufuta leseni ya kumiliki makao” Dkt. Gwajima.
Pia amewataka wamiliki wa makao hayo kuwaruhusu bila vipingamizi
Maafisa Ustawi wa Jamii kuingia makaoni na kufanya ukaguzi wakati wowote
inapohitajika ila kuhakikisha vigezo na taratibu zote zinazohitajika kufuatwa
na makao zinafuatwa ipasavyo.
Akisisitiza kuhusu hatma ya huduma kwa mtoto aliyeko kwenye
makao, Dkt. Gwajima amesema kila mmiliki wa makao anatakiwa kuhakikisha watoto
anaowalea wananufaika na huduma za makao na kuandaliwa kuunganishwa na familia
au jamii kupitia Malezi ya Kambo au kuasiliwa na au kuwezeshwa kujitegemea kwa
wale waliofikia umri na kujengewa uwezo.
Aidha, Dkt. Gwajima ametoa siku 90 kwa wamiliki wa makao ya
watoto kote nchini kuhakikisha wanahuisha Kamati za Makao na miezi sita kwa
kila mwenye makao kuwa amekamilisha taratibu zote za umiliki na uendeshaji wa
makao, vinginevyo wawasiliane Wizara moja kwa moja iwapo watakumbana na
changamoto.
Katika hatua nyingine Dkt. Gwajima amewapongeza na kuwatia
moyo wanaoendesha Makao ya Watoto kwa kufuata taratibu za uendeshaji na
kuongeza kuwa, Wizara inakamilisha Mapitio ya Mwongozo wa Uanzishaji na
Uendeshaji wa Makao ya Watoto na inatarajia kutoa toleo jipya Septemba 2023,
ili kuimarisha ulinzi wa watoto kwa kila nyanja.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia,
Wanawake na Makundi Maalum Dkt. John Jingu amesisitiza wamiliki wa vituo hivyo
kuzingatia sheria, taratibu na kanuni za usajili na uendeshaji wa makao na
kwamba, Wizara itaimarisha ufuatiliaji wa makao yote nchini ambayo kwa sasa
yako jumla 431 huku 58 yakiwa mkoa wa Dar es Salaam.
Nao wamiliki wa makao ya watoto mkoa wa Dar es Salaam
wakiongozwa na Mwenyekiti wao Bw. Evans Tegete, wamepongeza juhudi za Serikali
za kuwa na jukwaa la pamoja la mawasiliano ambalo litawasaidia kwenda pamoja
kwenye kuboresha hatua za maendeleo na ustawi wa watoto kwenye makao mbalimbali
nchini.
Na WMJJWM, DSM
0 Maoni