STAMICO kuwanunulia mitambo 15 wachimbaji wadogo

 

Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) linafanya jitihada mbalimbali za kuwaendeleza wachimbaji wadogo wa madini nchini kwa kuwapatia elimu pamoja na kuwanunulia mitambo ya kisasa ya uchimbaji.

Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO CPA, Dkt. Venance Mwasse, amesema katika utafiti walioufanya wamebaini wachimbaji wadogo wanakabiliwa na ukosefu wa taarifa sahihi za mashapo, teknolojia duni, kutokuwa na mitaji/kutokopesheka na kukosa masoko.

Akiongea na Wahariri leo, CPA, Dkt. Mwasse amesema STAMICO imenunua mitambo mitano ya kufanyia uchorongaji maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo, na kuongeza kwamba mitambo hiyo inatarajiwa kufika nchini mwezi Septemba 2023.

"Licha ya kununua mitambo hiyo mitano ya uchorongaji kwa wachimbaji wadogo, pia STAMICO itafanya ununuzi wa mitambo mingine 10, ambapo ifikapo mwishoni mwa mwaka wa fedha 2023/24 jumla ya mitambo 15 itakuwa imenunuliwa," amesema CPA, Dkt. Mwasse.

Ameongeza kuwa STAMICO itaanzisha vituo vya mfano vya kujifunzi teknolojia vyenye tija ya uchimbaji katika maeneo ya Lwamgasa, Katente na Itumbi, ambavyo vitawasaidia wachimbaji wadogo.

Akiongelea mafanikio ya STAMICO CPA, Dkt. Mwasse amesema kwamba wamefanikiwa kuongeza mapato ya ndani kutoka shilingi bilioni 1.3 kwa mwaka 2018/19 hadi kufikia shilingi bilioni 61.1 kwa mwaka 2022/23.

Pamoja na mambo mengine amesema kuwa shirika hilo limefanikiwa kutoka katika kujiendesha kwa hasara hadi kujiendesha kwa faida na kufanikisha kulipa gawio la serikali la jumla ya shilingi bilioni 8, na kuondoka kabisa katika utegemezi.

Chapisha Maoni

0 Maoni