PSSSF yawalipa sh bilioni 35 watumishi 13,000 waliotimuliwa kwa vyeti feki

 

Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), umelipa kiasi cha shilingi bilioni 35 kwa waliokuwa watumishi wa umma zaidi ya 13,000, waliofukuzwa kazi katika sakata la vyeti feki, ambao malipo yao yametokana na huruma ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa watumishi hao.

Rais Samia Suluhu Hassan alitoa agizo hilo katika Siku ya Wafanyakazi Duniani Mei Mosi ya mwaka 2022, ambapo aliagiza kuwa walioondolewa kwa vyeti feki enzi ya Serikali ya Awamu ya Tano walipwe stahiki zao kama mafao ya kustaafu, kwa kuwa watumishi hao waliutumikia umma.

Hayo yameelezwa leo na Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF CPA Hosea Ezekiel Kashimba, katika mkutano wake na Wahariri wa Vyombo vya Habari alipokuwa akielezea mafanikio ya PSSSF ndani ya miaka mitano, na kusema mfuko huo umebeba dhamana hiyo kwa kuwa waliofukuzwa kazi walikuwa ni watumishi wa umma.

“Katika kipindi cha miaka mitano PSSSF imefanya malipo ya mafao yanayofikia kiasi cha shilingi trilioni 8.88 kwa wanachama wake, kwa njia ya mafao mbalimbali yakiwemo malipo ya uzeeni, pensheni ya kila mwezi, mafao ya kifo, fao la kuacha kazi pamoja na mafao mengine,” amesema CPA Kashimba.

CPA Hosea pia amemshukuru Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha Serikali kulipa shilingi trilioni 2.17 ambayo ni malipo ya malimbikizo ya michango ya wanachama wa kabla ya Mwaka 1999 ya uliokuwa Mfuko wa PSPF, kati ya shilingi trilioni 4.6.

“Katika utekelezaji wa kipindi cha miaka mitano PSSSF imekusanya michango ya jumla ya shilingi trilioni 9.60, kiasi hiki kinajumuisha shilingi trilioni 2.17 ambayo ni malipo ya malimbikizo ya michango ya wanachama wa kabla ya mwaka 1999 ya uliokuwa Mfuko wa PSPF,” amesema CPA Kashimba.

Kuhusu uwekezaji unaofanywa na PSSSF CPA Kashimba amesema thamani ya uwekezaji imeongezeka kwa asilimia 23.5, kutoka shilingi trilioni 6.40 hadi kufikia shilingi trilioni 7.92, sawa na ongezeko la wastani wa 4% kwa mwaka.

Amesema mafanikio ambayo mfuko wa PSSSF umeyapata kwa kiasi kikubwa yamechangiwa na nia ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania.

CPA Kashimba ametumia mkutano huo kwa niaba ya Bodi ya Wadhamini wa Mfuko, kumshukuru Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, kwa uthubutu wake wa kuamua kulipa deni la michango la shilingi trilioni 4.6 la wanachama wa uliyokuwa Mfuko wa PSPF ya kabla ya Mwaka 1999, uamuzi ambao umewezesha Mfuko kulipwa kiasi cha shilingi trilioni 2.17 kupitia hatifungani maalum.

Serikali pia imelipa shilingi bilioni 500 katika deni la shilingi bilioni 731.4 la mikopo ya miradi ambayo mifuko iliyounganishwa iliikopesha Serikali ili kutekeleza miradi ikiwemo ujenzi wa; Jengo la Bunge, Chuo Cha Serikali cha Hombolo, Nelson Mandela Istitute of Science and Technology na Chuo Kikuu cha Dodoma.

Kuhusu uamuzi wa kuunganisha mifuko, CPA Kashimba amesema kwamba umekuwa wa manufaa kwa mfuko wa PSSSF, kwa kuuwezesha kujiendesha kwa ufanisi na kulipa mafao ya wanachama wake kwa wakati kutokana na kuongezeka kwa thamani ya mfuko.

Chapisha Maoni

0 Maoni