Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camilius Wambura ametoa
onyo kali kwa kundi la watu waliosambaza taarifa kuwa wanaandaa maandamano nchi
nzima juu ya kuiangusha Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa
Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassani kabla ya mwaka 2025.
IGP Wambura ametoa onyo hilo leo Jijini Dar es Salaam wakati
akizungumza na waandishi wa habari, na kusema cha ajabu wamehusisha maandamano
hayo wanayoyapanga kushawishi Watanzania kuwaunga mkono na hoja zinazoendelea za
mjadala wa bandari.
"Sisi tuliamini suala la bandari linajibiwa kwa hoja na
na vilevile tukaamini kwa sababu hawa watu walikwenda mahakamani wangeheshimu
maamuzi ya Mahakama lakini badala yake wametoka sasa na kuanza kutafuta
ushawishi na kuwataka Watanzania waingie kwenye maandamano ya nchi nzima na
miongoni mwao mmoja amekwenda mbali zaidi na kusema watahakikisha wanaangusha
Serikali ya Jamuhuri ya Muungano ya awamu ya sita," amesema IGP Wambura.
IGP Wambura amewasisitizia kwa kuwaonya vikali wasitishe
kabisa matamshi yao hayo ya kichochezi kwa kuwa watachukuliwa hatua kali za
kisheria kwa uhaini wanaotaka kuufanya kwani yote ni makosa ya jinai na Jeshi
la Polisi halitakaa kimya na kuwavumilia hicho wanachotaka kukifanya na kuvunja
amani iliyopo.
"Kama mfikiria tupo kimya basi tutakwenda kuwaonyesha
hatuko kimya kwa yeyote anayevunja sheria ya nchi hivyo niwatake Watanzania
wawapuuze watu hawa kwani Tanzania ni nchi ya amani na salama hawa wasitake
kuwashawishi na kuingiza nchi kwenye machafuko hatujawahi kufika huko na
hatutofika kwenye machafuko, " amesema IGP Wambura.
Aidha, wachochezi hao wametakiwa kutambua kuwa Jeshi la
polisi ni imara sana wasitikise kiberiti kama waliwahi miaka ya huko nyuma na wakaguswa
wasithubutu kwenda hatua nyingine huko wanakoshawishi kwenda ni sehemu mbaya
sana hivyo wananchi muwe watulivu muendelee kuishi kwa amani mkiendelea kufanya
shughuli zenu za kiuchumi kama ilivyokuwa desturi yenu.
CHANZO: UMG digital
0 Maoni