Naomba nifafanue hatujazuia kuuza mazao nje ya nchi- Rais Samia

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Samia Suluhu Hassan, amesema kwamba Serikali haijafunga mipaka uuzaji mazao nje ya nchi, bali ina lengo la kuwa na mfumo rasmi wa ununuzi, uuzaji na usambazaji wa mazao utakaoweza kutambua kiasi cha mazao yanayouzwa nje ya nchi.

Akiongea leo kwenye sherehe za kilele cha Siku ya Nanenane Jijini Mbeya, Mh. Samia amesema kwamba kwa hali ilivyo sasa Serikali haitambui kiasi halisi cha chakula kinachouzwa nje kutokana na wanunuzi wa nje kwenda moja kwa moja kwa wakulima na kununua mazao.

“Uzoefu uliopo sasa nikwamba magari yanatoka tu nchi jirani yanaingia moja kwa moja kwenye mikoa yetu, moja kwa moja kwenye wilaya zetu hayaulizwi yanakwenda mpaka kwa wakulima yananunua mazao na pale wanakwenda kulipa fedha zetu na wala hatupati fedha za kigeni,” alisema Mh. Samia.

Tukiweka mfumo mzuri wa ununuaji, tukidhibiti magari yanayokwenda moja kwa moja kununua kwa wakulima tutajua tunanunuaje na tunauzaje, “Ndio maana mwaka huu nikakupa fedha nyingi Mheshimiwa Waziri Bashe ili NFRA inunue mazao kwa wakulima tuyahifadhi ghalani ili watu wa nje waje kununua mazao hayo, lakini hakuna mkulima kuuza mazao moja kwa moja”.

Pia, Rais Samia amesema Serikali imeendelea kufanya jitihada za makusudi za kuongeza ushiriki wa vijana katika kilimo pamoja na wanawake, miongoni mwa jitihada hizo ni kuanzishwa kwa programu ya miaka minane ya kilimo inayojulikana kama Jenga Kesho iliyo Bora ama Bulding A Better Tomorrow (BBT).

“Hadi sasa vijana waliokidhi vigezo 812, wanawake 282 na wanaume 530 wanaendelea na awamu ya kwanza ya mafunzo ya kilimo au kilimo biashara katika vituo hatamizi 13 ambayo yanatolewa kwa miezi minne, baada ya hapo watapatiwa mashamba yanafofikia hadi hekari 10 na yatakodishwa kwao kwa miaka 66,” alisema Rais Samia.

Katika kuhakikisha mbolea inamfikia mkulima kwa bei nafuu hadi katika ngazi ya Kata, Rais Samia amemuagiza Waziri wa Kilimo Mh. Hussein Bashe kukutana na Waziri wa Fedha Dk. Mwigulu Nchemba kuona namna Serikali itakavyosaidia kupunguza gharama za usafiri ili kutombebesha mzigo mkulima.

Rais Samia pia amekumbushia tena agizo lake alilolitoa mwaka 2022 siku kama ya leo la kutaka kufanyika maonesho ya kilimo katika mikoa yote nchini ikiwa ni pamoja na kutenga viwanja vya maonesho ya Nanenane, ili kuchochea kasi ya ukuaji wa kilimo nchini.

Kwa upande wake Waziri wa kilimo Mh. Husein Bashe ameishukuru Serikali kwa kutoa ruzuku ya mbolea ambapo kwa mwaka huu serikali itatoa zaidi ya shilingi bilioni 200 kama ruzuku na kuongeza kwamba matumizi ya mbolea yataongezeka na kufikia tani 951000.

Kuhusu programu ya Jenga Kesho iliyo Bora (Bulding A Better Tomorrow) Mh. Bashe amesema kwamba kwa mara ya kwanza vijana wakitanzania watapatiwa umiliki wa ardhi, nyumba na mashamba kwa ajili ya kilimo na awamu ya kwanza itakuwa tarehe 20/08/2023.

Mhe. Bashe pia ameonekana kukerwa na vitendo vya uvamizi wa maeneo ya utafiti na mashamba ya mbegu na kuwataka wavamizi kuacha mara moja kufanya hivyo kwani hakuna maendeleo ya kilimo yatakayoweza kufikiwa bila ya uwepo wa mashamba ya mbegu.

Katika sherehe hizo Mh. Rais Samia Suluhu Hassan alitoa tuzo kwa mikoa iliyoongoza kwa uzalishaji mazao ya nafaka ya Ruvuma, Rukwa na Mbeya pamoja na ile ilioyoongoza kwa mazo yasiyo ya nafaka ya Kagera, Kigoma na Mbeya.

Chapisha Maoni

0 Maoni