Waziri Dkt. Mabula ashiriki kuaga miili ya waliogongwa wakifanya mazoezi

 

Mbunge wa Jimbo la Ilemela na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt Angeline Mabula amewaongoza mamia ya wakazi wa mkoa wa Mwanza kuaga miili ya watu watano kati ya sita waliofariki kwa kugongwa na gari wakifanya mazoezi ya kukimbia (Jogging) eneo la Lumala wilayani Ilemela mkoani Mwanza.

Katika ajali hiyo iliyotokea jumamosi Julai 22, 2023 na kuhusisha gari aina ya Hilux Double Cabin katika barabara ya Kiseke eneo la Lumala wilayani Ilemela ambapo dereva wa gari hiyo akiendesha kwa mwendokasi aliwagonga wana kikundi cha Adden Palace Jogging zaidi ya 30 na kusababisha vifo 6 na majeruhi 16.

Shughuli ya kuaga miili hiyo imefanyika tarehe 24 Julai 23, 2023 katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza ya Sekou Toure ambapo miili iliyoagwa ni ya Makorongo Manyanda unaosafirishwa kwenda Kahama mkoani Shinyanga, Peter Fredrick (Kigoma), Shedrack Safari (Kilimanjaro), Selestine Daudi (Mwanza) na Hamis Waziri (Geita).

Aidha, mwili wa marehemu Amani Magabe (24) uliotambuliwa jana tarehe 23 Julai 2023 na ndugu zake ulichukuliwa na kusafirishwa kuelekea wilayani Tarime mkoani Mara kwa ajili ya Maziko.

Akizungumza baada ya ibada ya kuaga miili hiyo, Dr Mabula amesema vifo vya marehemu hao viliishtua Serikali na kusema kuwa, kama mbunge na mtunzi wa sheria anaona kuja haja kufanya mapitio ya sheria ya usalama barabarani ili wanaosababisha ajali na kupelekea vifo kwa makusudi washtakiwa kwa kesi ya mauaji badala ya kesi ya trafiki.

Pia amevitaka vikundi vya wafanya mazoezi ya kukimbia kuongeza umakini wanapofanya mazoezi sambamba na kuzitaka mamlaka kuhakikisha aliyesababisha ajali hiyo anachukuliwa hatua.

Hafla ya kuaga miili hiyo imehudhuriwa na kushuhudiwa na ndugu, jamaa, marafiki na mamia ya wakazi wa mkoa wa Mwanza wakiongozwa na vikundi mbalimbali vya wafanya mazoezi mkoani humo.

Vile vile, Dkt Mabula aliwatembelea majeruhi wa ajali hiyo waliolazwa katika hospitali za Bugando na Sekou Toure jijini Mwanza ambapo aliwatia moyo na kuwaombea wapote haraka ili waweze kuendelea na majukumu yao.

Chapisha Maoni

0 Maoni