Watatu washikiliwa kwa kumtorosha mwanafunzi ili aolewe

 


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linawashikilia watuhumiwa watatu 1. NAZARETH NDELE [50] 2. STEVEN MWAIGAGA [29] na 3. FARAJA MWAIGAGA [26] wote wakazi wa Kijiji cha Igunda Wilaya ya Mbeya Vijijini kwa tuhuma za kumtorosha mwanafunzi na kutaka aolewe na kijana wao kinyume cha sheria.

Ni kwamba Juni 12, 2023 huko Kijiji cha Santilya, Mwanafunzi wa Kidato cha Nne katika Shule ya Sekondari Santilya (jina linahifadhiwa) mwenye umri wa miaka 17 alikutana na CHANDE MWAIGAGA ambaye alimshawishi na kuingia naye kwenye mahusiano ya kingono.

Julai 20, 2023 mtuhumiwa CHANDE MWAIGAGA alimfuata mwanafunzi huyo kwenye makazi aliyokuwa amepangishiwa na baba yake mzazi aitwaye MAJALIWA MISTON [46] Mkazi wa Kijiji cha Jojo – Mbalizi kutokana na umbali wa kutoka nyumbani hadi shuleni na kisha kuondoka naye kwenda kuishi naye kinyumba Kijiji cha Ilindi Wilaya ya Mbeya Vijijini.

Julai 27, 2023 saa 3:00 asubuhi, MAJALIWA MISTON [46] akiwa nyumbani kwake Kijiji cha Jojo alipokea ugeni wa watu watatu ambao ni NAZARETH NDELE [50], STEVEN MWAIGAGA [29] na FARAJA MWAIGAGA [26] ambao walijitambulisha kwake kuwa wao ni washenga wa CHANDE MWAIGAGA ambaye anaishi na binti yake na kueleza lengo lao ni kutoa posa Tshs.110,000/=, Mahali Ng’ombe mmoja, Mbuzi Jike mmoja, Blanket moja na mashuka mawili.

Kufuatia hali hiyo, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya lilipata taarifa na kufika eneo la tukio na kutokana na ushirikiano na Mtendaji wa Kata, Mwenyekiti wa Kijiji na Wananchi, Jeshi la Polisi lilifanikiwa kuwakamata watuhumiwa wote watatu ambao baadae waliowezesha kupatikana kwa binti huyo akiwa nyumbani kwa mtuhumiwa. Jitihada za kumtafuta mtuhumiwa CHANDE MWAIGAGA zinaendelea.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linatoa wito kwa vijana kuacha tabia ya kuwalaghai na kuwarubuni wanafunzi kitendo ambacho ni kinyume cha sheria na kinachosababisha kuwaharibia masomo. Aidha, Jeshi la Polisi linatoa rai kwa wazazi/walezi kuacha kusaidia/kuungana na watoto wao katika vitendo vya uhalifu.

Imetolewa na:

BENJAMIN KUZAGA

Kamanda wa Polisi,

Mkoa wa Mbeya.

Chapisha Maoni

0 Maoni