Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma
na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema taaluma ya Uuguzi ni kazi ya
uthubutu, utayari pamoja na kujitoa kwa ajili ya kuwahudumia wenye mahitaji ya
kiafya huku akiwataka Wauguzi kuendelea kuchapa kazi kwa weledi na kwa
kuzingatia miiko na maadili ya taaluma yao.
Mhe. Kikwete ameyasema hayo leo Jumapili Julai 23, 2023
wakati akizungumza na Wauguzi wa Mkoa wa Pwani kwenye Kilele cha Maadhimisho ya
Siku ya Wauguzi Duniani yaliyofanyika kimkoa katika Halmashauri ya Wilaya ya
Chalinze ambapo amewahimiza Wauguzi hao kuwahudumia wananchi kwa moyo na upendo
wa hali ya juu.
Amesema, Serikali inatambua kuwa Wauguzi ni kundi muhimu
sana kwani ndio shina na mhimili mkubwa wa utendaji na ufanisi wa sekta ya afya
nchini na ulimwenguni kote.
Mhe. Kikwete ametumia fursa hiyo kumshukuru Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka
mazingira mazuri ya kufanyia kazi Wauguzi hao ikiwa ni pamoja na kuweka
mikakati mbalimbali ili kuyafikia malengo endelevu ya afya kwa wote.
Aidha, Mhe. Kikwete amesema Ofisi ya Rais-UTUMISHI inaendelea
kuzifanyia kazi changamoto za kimuundo za taaluma hiyo na changamoto nyingine
itaishirikisha Wizara husika ya Afya ili ziweze kufanyiwa kazi.
Katika hatua nyingine, Mhe. Kikwete amekubali ombi la kuwa
mlezi wa Wauguzi katika Mkoa wa Pwani huku akiahidi kuwapa ushirikiano ili
kuwaongezea morali Watumishi hao katika kutekeleza majukumu yao.
‘’Natambua mchango wenu adhimu kwa mustakabali wa afya zetu
kwani ziko mikononi mwenu, napenda kuwaahidi mimi kama mlezi wenu niko tayari
kuwapa ushirikiano muda wote mtakaponihitaji,” amesisitiza Mhe, Kikwete.
Awali, Katibu wa Chama cha Wauguzi Mkoa wa Pwani, Bi.
Dafroza Mnzava akisoma risala kwa Naibu Waziri Mhe. Kikwete, ameiomba Serikali
kuzifanyia kazi changamoto zinazowakabili ikiwemo suala la muundo na posho ya
mazingira hatarishi na stahiki mbalimbali.
Pia Katibu huyo ameiomba Serikali kuendelea kuajiri wauguzi
ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
Maadhimisho hayo yenye kauli mbiu “WAUGUZI WETU, MUSTAKABALI
WA AFYA ZETU” yamefanyika mkoani humo ikiwa ni kuenzi kumbukumbu ya Muasisi wa
Uuguzi na Ukunga Duniani, Bi. Florence Nightingale wa nchini Italia, aliyejitoa
kwa moyo kuwahudumua wenye mahitaji ya kiafya.
Na. Lusungu Helela-Chalinze
0 Maoni