Makumbusho kushirikisha jamii katika kuhifadhi utamaduni

 

Makumbusho ya Taifa la Tanzania itaendelea kushirikisha jamii na wadau katika wajibu wa kuhifadhi Urithi wa asili na utamaduni wa Tanzania kwa kuweka uwiano sawa wa jamii kuifikia Makumbusho kwa kushirikisha makundi mbalimbali yakiwemo ya Watoto wenye uhitaji maalum katika program zitakazoisogeza jamii karibu zaidi na Makumbusho.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa la Tanzania, Dkt. Noel Lwoga wakati wa maadhimisho ya Siku ya Utamaduni wa Mtanzania na Ujerumani yaliyofanyika Kijiji cha Makumbusho kilichopo Kijitonyama jijini Dar es Salaam yaliyohudhuriwa na vijana kutoka nchini Ujerumani na Watoto wenye uhitaji maalum kutoka eneo la Manzese jijini Dar es salaam wanaofadhiliwa na taasisi ya Youth Crossing Boundaries Foundation.

Dkt.Lwoga amesema kupitia matukio haya jamii inaweza kujifunza na kubadilishana uzoefu wa tamaduni mbalimbali na hatimaye kujenga uelewa wa pamoja wa tofauti za tamaduni na hatimaye kuleta amani katika jamii hususan kwa watoto wenye uhitaji maalum ambao aghalabu hukosa fursa ya kujifunza masuala mbalimbali.

Kwa upande wake Mwanzilishi wa Taasisi ya Youth Crossing Boundaries, Father. George Rupperecht kutoka nchini Ujerumani amesema lengo ni kuwapatia haki ya elimu Watoto wenye uhitaji maalum kuanzia ngazi ya elimu ya msingi mpaka vyuo vikuu.

Amesema kuwa kupitia tukio hili katika Makumbusho ya Taifa Watoto wataweza kujifunza utamaduni wao na kupata uzoefu wa tamaduni zingine ili kukuza uelewa wao kuhusu masuala ya Utamaduni.

Chapisha Maoni

0 Maoni