Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, CP Benedict Wakulyamba amelisisitiza Jeshi la Uhifadhi, Wanyamapori na Misitu kulinda Maliasili za nchi ili kuwavutia watalii wengi zaidi wanaotembelea nchini na kuliwezesha taifa kupata mapato mengi yanayotokana na utalii kwa Maendeleo ya nchi.
Aliyasema
hayo hivi karibuni alipokuwa akizungumza na Watumishi wa Hifadhi ya Taifa
Katavi iliyopo mkoani Katavi. CP Wakulyamba alisema
"Jukumu la Jeshi hili ni kulinda
maliasili ili kuvutia watalii wengi zaidi na kukuza pato la taifa, na jukumu
hili tumepewa kisheria hivyo ni wajibu wa kila mmoja kutekeleza kazi hizo kwa
kufuata sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa."
Hata
hivyo, CP Wakulyamba alizitaka taasisi zilizo chini ya Wizara ya Maliasili na
Utalii kuongeza ushirikiano tofauti na ilivyo sasa. Katika kuthibitisha hilo
alisema, "inaonekana hakuna ushirikiano wa kutosha baina yenu, hivyo ni
lazima mshirikiane ili muwe na umoja thabiti maana ulinzi wa maliasili
unahitaji nguvu ya pamoja. Pia shirikianeni na majeshi mengine kama vile Jeshi
la Wananchi wa Tanzania, Polisi, Uhamiaji na Magereza kwa sababu kazi zenu
zinategemeana".
Naye,
Naibu Kamishna wa Uhifadhi TANAPA Steria Ndaga, Mkuu wa Kanda ya Kusini
alimpongeza CP Wakulyamba kwa kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya
Maliasili na Utalii na kumuaidi kumpa ushirikiano pamoja na kutekeleza maagizo
yote aliyoyatoa.
Pia,
Kamishna Ndaga alimshukuru CP Wakulyamba kwa ziara ya kikazi katika Hifadhi ya
Taifa Katavi inayosifika kwa kuwa na viboko wengi, pia alielezea mafanikio
yanayoendelea kuonekana baada ya Uzinduzi wa Filamu maarufu duniani ya “Tanzania
Royal Tour” iliyoasisiwa na Mhe. Rais Samia
CP
Wakulyamba alifanya kikao na Maafisa na Askari wa Jeshi la Uhifadhi kutoka TAWA
na TFS.
Na.
Jacob Kasiri - Katavi.
0 Maoni