WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemtaka Mganga Mkuu wa Wilaya ya
Mtwara, Dkt. Matayo Malaika ahakikishe anasimamia ujenzi wa kituo cha afya
Mkunwa ili kikamilike ifikapo Oktoba, 2023.
Ametoa agizo hilo jana (Jumamosi, Julai 8, 2023) wakati
akizungumza na wananchi wa kata ya Mkunwa mara baada ya kukagua ujenzi wa kituo
hicho, kilichopo Halmashauri ya Mtwara Vijijini, mkoani Mtwara.
“Nimekagua ujenzi wa kituo hiki cha afya, nimekuta vifaa
vimejaa humo ndani, rangi, masinki ya mikono, vyoo, gutters, marumaru, saruji,
vyote vipo na vinataka kuharibika. Mganga Mkuu simamia huu ujenzi na umshauri
vizuri Mkurugenzi. Nataka hatua zote zilizobakia zikamilishwe na hapa ni lazima
pawe na watu sababu kuna mali za umma,” amesisitiza.
“DMO mnakaa sana ofisini badala ya eneo la ujenzi, simamia
kituo cha afya hiki kikamilike, una vituo vya afya vitatu na hiki ni cha nne,
milango imekaa tu, jengo lipo kwa nini usiweke hii milango kwenye maeneo yake?,”
alihoji Waziri Mkuu.
Amemtaka Mhandisi wa Halmashauri hiyo ashirikiane na Mganga
Mkuu huyo kuandaa mapitio ya mradi na wapeleke maombi yao Ofisi ya Rais
TAMISEMI ili waweze kupatiwa fedha za kukamilisha majengo ya kituo hicho
ambacho amesema kinapaswa kuwa na hadhi ya hospitali ya Halmashauri kutoka na
umaalumu uliopo.
“Kwa sababu hapa kuna vyumba vingi, angalieni uwezekano wa
kuwa na chumba cha upasuaji cha wagonjwa wa kawaida tofauti na kile kilichopo
kule kwenye jengo la akinamama. Pia katika mapitio yenu, wekeni wodi tatu
ikiwemo wodi ya wanaume, wodi ya wanawake na ya magonjwa mchanganyiko,”
amesisitiza.
Amewataka wakamilishe ujenzi huo kwa sababu tayari Serikali
ilishatenga sh. milioni 300 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba vya kituo hicho.
Mapema, akitoa taarifa ya ujenzi kwa Waziri Mkuu, Dkt.
Malaika alisema mradi huo ukikamilika utahudumia vijiji sita vya kata ya Mkunwa
na kata jirani za Mayanga, Muungano na Dihimba.
Alisema Septemba, 2021 Halmashauri ilipokea shilingi milioni
250 kwa ajili ya jengo la wagonjwa wa nje (OPD), maabara na kichomea taka.
“Juni, 2022, Halmashauri ilipokea fedha za awamu ya pili shilingi milioni 250
kwa ajili ya wodi ya wazazi na jengo la upasuaji, njia ya kutembelea na jengo
la kufulia yenye hadhi ya kituo cha afya”.
Alisema kutokana na maamuzi ya kuhamishia hospitali ya wilaya
kwenya kata ya Nanguruwe, Halmashauri iliomba kibali cha kubadilisha matumizi
ili kuendeleza ujenzi wa wodi ya wazazi na jengo la upasuaji vyenye hadhi ya
Hospitali ya Wilaya ambapo ujenzi wake ulianza Novemba, 2022.
“Kwa sasa ujenzi upo hatua ya ukamilishaji na kazi
zinazoendelea ni skimming, ufungaji wa gypsum boards, uwekaji wa fremu za
milango na ujenzi wa marumaru”.
Majengo mengine ambayo yalianza kujengwa na yako kwenye hatua
ya msingi ni jengo la mionzi, la maabara na la kufulia.
Chanzo: Ofisi ya Waziri Mkuu
0 Maoni