Serikali imesema, imeandaa hatua na mikakati madhubuti yenye
kuibua fursa za miradi ya kijamii kwa wananchi, ikiwemo kanuni na mwongozo wa
biashara ya kaboni ikiwa ni njia mbadala ya kukabiliana na athari za mabadiliko
ya tabianchi.
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 19 Juni 2023 na Naibu Katibu
Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Abdallah Hassan Mitawi wakati akifunga warsha ya
siku moja baina ya wahariri na menejimenti ya ofisi hiyo, iliyolenga kujenga
uelewa kuhusu kanuni na mwongozo wa biashara ya kaboni.
Mitawi amesema, Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazoathiriwa
na athatri za mabadiliko ya tabianchi na hali ya hewa isiyotabirika hali
inayojidhihirisha kupitia matukio ya mvua zisizotabirika, ongezeko la joto,
ukame na mafuriko, ambapo athari hizo zimeathiri sekta za kijamii na kiuchumi.
“Pamoja na changamoto zinazochangiwa na mabadiliko ya tabia
nchi kumekuwa na fursa na jitihada mbalimbali ambazo zimechukuliwa na serikali
ikiwa ni pamoja na mapitio ya sera, uandaaji wa kanuni, mikakati na miongozo ya
kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi,” amesema Mitawi.
Chanzo: editorsforums
0 Maoni