Transfoma za Tanesco haziogopi mvua, tatizo ni waya hazina ganda la nje

 

Mkurugenzi wa Shirika la Umeme nchini (Tanesco), Maharage Chande, amesema wanalazimika kukata umeme inaponyesha mvua kubwa ili kuepusha madhara kutokana na waya za umeme wanazotumia kutokuwa na (insulator) ganda la nje la plastiki la kuzuia maji ya mvua yasisababishe hitilafu.

Bw. Chande amebainisha hayo jana usiku Dar es Salaam wakati akijibu maswali ya wahariri wa vyombo vya habari katika majadiliano yaliyofanyika kujadili sekta hiyo ya umeme na kuelezea mafanikio na mipango ya shirika la Tanesco.

Mkurugenzi huyo amesema kwamba sio kweli kama transfoma zao zinaogopa mvua ama radi, bali ukweli ni kwamba waya wanazotumia hazina maganda ya kuzilinda hivyo mvua kubwa inaponyesha inaweza kusababisha hitilafu ya umeme.

“Waya tunazotumia kwa sasa hazina ganda la nje la (insulator), sasa mvua ikinyesha kubwa maji yanasababisha muunganiko wa waya na kupelekea kutokea shoti ya umeme na kuathiri miundomninu,” alisema Bw. Chande na kuongeza “Waya zenye ganda ni ghali mno”.

Ukusanyaji madeni ya umeme

Akiongelea suala la ukusanyaji wa madeni ya umeme kwa wateja wao wanaodaiwa, Bw. Chande amesema Tanesco imeshatangaza tenda ya kuwapata wataalam wa kudai madeni na tayari mshindi ameshapatikana.

“Tumetangaza tenda ya kuwapata wababe wa kudai madeni na tayari mshindi amepatikana, hivi karibuni ataanza kazi mtasikia heka heka, na sisi Tanesco tupo tayari kwa yatakayotokana na heka heka hizo,” alisema Bw. Chande.

Umeme wa Jua

Kuhusu matumizi ya umeme wa jua, Bw. Chande amesema jumatato ya wiki ijayo Tanesco wanatarajia kutia saini mradi mkubwa wa uzalishaji umeme wa jua, ambao ni mkubwa kuwahi kufanyika katika nchi za Afrika Mashariki.

“Jumatatu ya wiki ijayo Tanesco tutatia saini mradi wa umeme wa jua wa Megawati 50, nadhani huu utakuwa ni moja ya mradi mkubwa wa umeme wa jua kuwahi kufanyika kwenye nchi za Afrika Mashariki,” alisema Chande huku akionyesha hisia za kujivunia mradi huo mkubwa.

Amesema mradi huo wa umeme wa jua utafanyika huko Kishapu, Shinyanga ambapo umeme wake utaingizwa kwenye gridi ya taifa ifikapo Julai 2024. Kwa sasa Tanesco inazalisha Megawati 5 tu za umeme wa jua zinazotumika katika mkoa wa Kigoma.

Matumizi ya Teknolojia

Kuhusu Tanesco katika kuchangamkia matumizi ya teknolojia Bw. Chande amesema wamekuwa wakishughulikia suala la kuwa na mita janja (smart meter) walizopata awali zilikuwa ghali lakini kwa sasa wamepata mita janja ambazo ni nafuu.

“Tumekuwa tukipanga kuanza kutambulisha mita janja, lakini kwanza tulipata mita ambazo ni ghali sana, ila sasa tumepata mita janja nafuu hata hivyo mita hizo zinahitaji pia kuwa na mfumo wake wa kuwasiliana na mita ambao nao unagharama zake,” alisema Bw. Chande.

Pamoja na mambo mengine, Bw. Chande amesema kwamba Tanesco inafikiria kuanza kutumia magari yanayotumia nishati ya umeme, ili kupunguza gharama za matumizi ya magari wanayotumia sasa ambayo yanatumia mafuta ya dizeli.

Chapisha Maoni

0 Maoni