Waziri wa Mambo ya Ndani wa Kenya Prof. Kithure Kindiki ameelezea
vifo vya waumini wa dhehebu la dini ya Kikristo eneo la Shakahola kuwa ni
uhalifu uliopangiliwa.
Waziri huyo ametoa kauli hiyo leo alipowasili Malindi mkoa
wa Pwani kusimamia zoezi la kufukua makaburi, ambalo lilisitishwa wiki
iliyopita kutokana na hali mbaya ya hewa.
“Ninahofia kwamba tuna makaburi mengi,” Prof. Kindiki
alisema na kuongeza kwamba ufukuaji wa makaburi unaweza kuchukua muda mrefu
kuliko ilivyotarajiwa.
“Uharibifu uliofanywa upo dhahiri, makaburi 20 walimozikwa
watu wengi kwa sasa yamefukuliwa. Mchakato wa kufukua makaburi sio wa kuisha
hivi karibuni,” alisema Prof. Kindiki.
Hadi sasa miili ya watu 112 hadi sasa imepatikana na vifo
vyao vimethibitishwa, huku Mchungaji wao Paul Mackenzie, na mchungaji mwingine
Ezekiel Odero wakiendelea kushikiliwa na polisi.
0 Maoni