WMA wakagua usahihi wa vipimo kwenye viwanda vya mabati mkoani Mwanza

Na. WMA - Mwanza

Wakala wa Vipimo (WMA) Mkoa wa Mwanza umezitaka kampuni zinazojihusisha na uzalishaji wa mabati kuhakikisha zinazingatia matakwa ya sheria ya vipimo na viwango vya ubora vilivyowekwa, ili kulinda haki na fedha za wananchi.

Akizungumza mapema leo Agosti 27, 2026 mara baada ya zoezi la ukaguzi wa kushtukiza katika baadhi ya viwanda vya uzalishaji wa mabati mkoani Mwanza, Meneja wa Mkoa wa Wakala huo, Karim Zuberi, amesema kupitia kaguzi na taarifa zinazotolewa na wananchi, ndani ya kipindi cha mwaka huu, tayari wamebaini na kuchukua hatua dhidi ya wazalishaji watano waliobainika kuzalisha mabati yasiyokuwa na vipimo sahihi.

Zuberi amesema wananchi wanapaswa kuwa makini wanaponunua mabati na kutoa taarifa kwa mamlaka husika pindi wanapohisi kuuziwa bidhaa zisizokuwa na vipimo sahihi, akiwataka pia wafanyabiashara kuacha tabia ya kuwapotosha wateja kuhusu vipimo vya unene wa mabati.

Amesema baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakitoa taarifa zisizo sahihi kwa wateja kwa kuwafanya waamini kuwa kadri namba ya 'Gauge' inavyokuwa kubwa ndivyo bati linavyokuwa bora, wakati kinyume chake ndicho sahihi, ambapo bati lenye namba ndogo ya "Gauge' huwa na unene mkubwa zaidi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wananchi kupata taarifa sahihi kuhusu viwango vya bidhaa wanazonunua ili kuepuka udanganyifu unaoweza kusababisha hasara, hususan katika ujenzi wa makazi na miundombinu mingine.

Kwa upande wake, Biyolelo Ndaisaba, mmoja wa viongozi wa kampuni inayojihusisha na uzalishaji wa bidhaa hizo mkoani Mwanza, amesema udanganyifu katika vipimo vya mabati ni sawa na kuhujumu jasho la wananchi wanaotumia fedha zao kujenga makazi na kuendeleza shughuli nyingine.

Amesema kampuni yao imeendelea kuwa kinara katika kuzingatia usahihi wa vipimo vinavyotakiwa kisheria, akisisitiza kuwa wazalishaji wote wana wajibu wa kuhakikisha bidhaa wanazozipeleka sokoni zinakidhi viwango kwa manufaa ya walaji.

Wakala wa Vipimo Mkoa wa Mwanza unaendelea na zoezi la ukaguzi wa bidhaa mbalimbali, linalofanyika kwa utaratibu wa kawaida pamoja na ukaguzi wa kushtukiza, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha wananchi wanalindwa dhidi ya bidhaa zisizokidhi vipimo sahihi.



Chapisha Maoni

0 Maoni